Na MAGDALENE WANJA
PATRICK Mugambi alianza biashara yake mnamo mwaka 2014 alipokuwa bado ameajiriwa katika kampuni ya kuundia wateja wavuti mbalimbali.
Katika muda huo, alikuwa akikutana na wateja wake wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana na jioni baada ya kazi yake ya mchana.
“Nilikuwa sina muda kabisa kwani nilikuwa nikifanya kazi hizi mbili zikiandamana, na wakati mwingi nilikuwa kwenye matatu nikienda kukutana na wateja kwenye mikutano mbalimbali,” anasema Patrick.
Ilifikia wakati ikaanza kuonekana kama kwamba kazi yake ya kuajiriwa ilikuwa inashindana na ile yake ya kando aliyokuwa akifanya. Jambo hili halikumfurahisha mwajiri wake.
“Mwaka 2014 ukikaribia kukamilika, mwajiri wangu aliniachisha kazi. Hapo niliona kuwa nilikuwa na nafasi ya kufanya kazi yangu bila matatizo,” akasema.
Kulingana na Patrick, kumiliki wavuti ni muhimu sana kwa biashara yoyote, kwani wateja wengi sasa wanapatikana mtandaoni.
“Kampuni yangu hutengenezea wafanyabiashara wavuti ili wapate nafasi nzuri ya kuuza huduma na bidhaa zao mitandaoni kwa urahisi,” anasema.
Anaongeza kuwa bei ya huduma zake hutegemea ‘ukubwa’ wa wavuti ambao huwa ni chaguo la mteja.
“Kwa mfano kuna wateja ambao huchagua domain ambazo wanalipia Sh800, huku wengine wakichagua za Sh1,200, na hivyo inategemea mteja anataka huduma ya aina gani,” anaeleza.
Kwa huduma za kutengenezewa wavuti, wateja hulipa kati ya Sh100,000 na Sh500,000. Ada hizi pia hutegemea na mahitaji ya mteja.
Patrick anaongeza kuwa baada ya kufanya kazi hii kwa muda, ameweza kujifunza jinsi ya kukabiliana na changamoto mbalimbali.