NA LABAAN SHABAAN
WABUNGE wa kambi tawala ya Kenya Kwanza, wamemtaka Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta kuvunja kimya kuhusu msimamo wake wa maandamano yanayopangwa kufanyika Jumatatu jijini Nairobi na muungano wa Azimio la Umoja – One Kenya.
Wakiongozwa na mbunge wa Naivasha, Jayne Kihara wamesema itakuwa busara kwa Bw Kenyatta kujieleza ikizingatiwa kwamba amenukuliwa akisema lililokuwa chaguo lake kumrithi linasalia kuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga.
Akionekana kumrushia Kenyatta cheche kali za maneno, alikiri kuwa hajawahi kumzungumzia hadharani lakini sasa anataka kujua msimamo wake kuhusu maandamano ya Azimio.
“Lazima tumuambie Uhuru Kenyatta, kama hayuko katika haya maandamano ajitokeze. Tumemsikia akisema Raila angali kiongozi wake na rais wake. Tunachosema ni kuwa kama unahusika na maandamano haya jitokeze na uongee,” mbunge huyo alisema.
“Mimi ni wa bonde la ufa ambapo tumeonja machafuko ya kisiasa. Ulipelekwa katika Mahakama ya Kimataifa (ICC) na karibu tuende na wewe. Jitokeze na utangaze msimamo wako kuhusu maandamano ya Azimio,” Bi Kihara alisisitiza.
Kwa moto uo huo kiongozi wa wengi katika bunge la kitaifa, Bw Kimani Ichungwa amedai kuwa Rais mstaafu huyo ni mfadhili mkubwa wa maandamano ya Jumatatu, ambayo kulingana na Raila yataelekezwa Ikulu ya Nairobi.
Walitaka kujua msimamo wa Kenyatta, wakati wakizungumza katika Shule ya Upili ya Wavulana ya Kianyaga, iliyoko Kaunti ya Kirinyaga ambapo Naibu Rais Rigathi Gachagua alizuru shule hiyo mnamo Jumamosi.
Bw Gachagua amefanya ziara kadha katika shule hiyo aliyosomea, ili kuwapa wanafunzi motisha.
Serikali aidha imetoa onyo kali kwa upinzani, endapo maandamano ya Jumatatu yatavuruga amani wahusika watachukuliwa hatua kisheria.