Na MAGDALENE WANJA
MNAMO mwaka 2020, Victor Kamau alitumia muda wake mwingi kufanya utafiti ili kupata dawa za kumtibu nduguye mdogo aliyekuwa akiugua kwa muda mrefu.
Juhudi za familia zote ziliambulia patupu kwani hata baada ya kutembelea hospitali mbalimbali, hawakuweza kubaini chanzo cha maradhi yake.
Alipokuwa akifanya utafiti wake, alichanganya aina ya matunda ya kiasili ambayo alimpa pia rafike yake wa karibu Bi Nduta Waidhima, aliyekuwa na changamoto ya kuwa na uzani wa kiwango cha juu.
Baada ya majuma matatu, Bi Waidhima alikuwa ameanza kupoteza uzani, na ngozi yake ilikuwa imeanza kulainika.
Kwa upande mwingine, nduguye Kamau alikuwa amepata nafuu zaidi.
“Nilitumia mchanganyiko wa poda ya moringa na mabuyu ambapo niliuchanganya na maji glasi moja na kuyanywa kila siku kwa kipindi fulani. Nilishangazwa sana na matokeo hayo,” akasema Bi Waidhima.
Wakati huo, Bi Waidhima alikuwa amepoteza kazi kutokana na janga la Covid-16, na marafiki wake walipoulizia kuhusu bidhaa za kiafya alizotumia, aliona kuwa ile ilikuwa fursa ya kufanya biashara.
Baada ya mashuriano, wawili hao waliamua kufanya biashara na wakafungua kampuni ya Gwin Organics iliyoanza kufanya shughuli zake katika mji wa Nakuru na wakaanza kuuza bidhaa hizo mtandaoni.
Baada ya muda mfupi, walifungua duka jijini Nairobi katika Kiambu Road.
“Tunatumia virutubisho mbali mbali ili kufikia viwango vinavyotakikana ili kutibu maradhi ya aina tofauti tofauti na kusawazisha homoni,” anasema Bi Waidhima.
Vile vile wanatengeneza juisi za aina tofauti za kutibu maradhi na zile za kukabiliana na hangover wakati wa asubuhi baada ya kulewa.
Glasi moja ya juisi huuzwa kwa Sh400, huku vifushi vya kutumia kwa muda mrefu vikipakiwa na kuuzwa kati ya Sh3,500 na Sh10,000.
Biashara hiyo huwahudumia wateja zaidi ya 400 kila mwezi.
Baadhi ya mimea wanayotumia ni pamoja na moringa, baobab, burdock root, spirulina na okra, ambayo hupatikana humu nchini, huku wakiagiza mingine kutoka nchi za nje. Ile inayoagizwa kutoka nje ni chlorella, seamoss, elderberry, ginseng na maca powder.