• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 8:55 AM
WANGARI: KNUT ishirikiane na serikali kuboresha maslahi ya walimu

WANGARI: KNUT ishirikiane na serikali kuboresha maslahi ya walimu

Na MARY WANGARI

MUUNGANO wa Kitaifa wa Walimu (KNUT) umekuwa ukikabiliwa na misukosuko tele inayotishia kuuzika katika kaburi la sahau.

KNUT ambayo kwa miaka mingi iliibua fahari miongoni mwa walimu waliokuwa wanachama wake, sasa imesalia kivuli tu cha hali yake ya awali huku ikigubikwa na sintofahamu kuhusu mustakabali wake.

Kuanzia ukosefu wa pesa, misururu ya kesi zinazoiandama, siasa kuhusu usimamizi zinasababisha mivutano ya kila mara kuhusu uongozi, ni bayana kwamba hali si shwari kabisa katika muungano huo.

Kando na hayo, kuchipuka kwa makundi hasimu kama vile Muungano wa Walimu wa Shule za Msingi Nchini (KUPPET), Muungano wa Walimu Wanawake Nchini (KEWOTA) na mengineyo, kumevuruga hali hata zaidi na kutishia kuvunjilia mbali kundi hilo.

Kwa kuzingatia historia ya sekta ya walimu nchini, ni vigumu kuamini kwamba miaka michache tu iliyopita, KNUT ilikuwa muungano mkuu uliozungumza kwa sauti imara na kusikika huku ukiwaunganisha walimu kote nchini.

Mwaka wa 2019 hususan ulikuwa mbaya zaidi kwa KNUT huku idadi ya wanachama wake ikipungua pakubwa kutoka zaidi ya 187,000 hadi 106,000.

Katibu Mkuu wa KNUT Wilson Sossion huenda ndiye aliyeathirika pakubwa kutokana na misukosuko katika muungano huo aliouongoza kwa muda mrefu huku akijitahidi kwa vyovyote kuzuia usizame.

Si ajabu kumwona akiwa amejawa na uchungu mwingi kila mara anapojitokeza kuzungumzia na kutetea maslahi ya KNUT.

Huku KNUT ikionekana kudidimia, Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC) inaonekana kuzidi kujiimarisha na kuchukua nafasi yake.

Hali hiyo ililazimu taasisi ya Elimu Kimataifa pamoja na Muungano wa Wafanyakazi Kimataifa (ITUC) kumwandikia barua Rais Uhuru Kenyatta ukimtaka aingilie kati kuhusu masaibu ya KNUT, ni picha halisi ya jinsi mambo yalivyo.

Hata hivyo, baadhi ya wachanganuzi wanahoji kwamba masaibu ya KNUT ni ya kujitakia.

Baada ya kunawiri kwa miaka mingi huku ikionekana kuwa na nguvu hata kushinda serikali inayowakilishwa na TSC, huenda KNUT ilipofushwa na ushindi wake wa kila mara.

Mashaka ya KNUT hasa yalianza 2013 huku ikionekana kushindwa kufanya kazi na serikali mpya iliyochukua usukani ambapo matokeo yake yalikuwa migomo ya kila mara ya walimu iliyotatiza sekta ya elimu.

Ni kweli kuna masuala tata yanayostahili kutatuliwa, hata hivyo, si jambo la busara kuruhusu KNUT kusambaratika kabisa.

Ni sharti usimamizi wa KNUT utilie maanani nafasi yake kama muungano wa kitaaluma, ukubali na kushirikiana na serikali katika kuboresha maslahi ya walimu.

Huenda bado kuna matumaini endapo wadau husika kutoka pande zote mbili watalegeza misimamo yao mikali na kushirikiana kutafuta suluhu.

[email protected]

You can share this post!

Mtambue ‘Madam Vicky’ wa kipindi cha...

TAHARIRI: Mzozo mpakani na Somalia utatuliwe