• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
STEVE ITELA: Wadau washirikiane kutatua changamoto za makao kwa wanyamapori

STEVE ITELA: Wadau washirikiane kutatua changamoto za makao kwa wanyamapori

Na STEVE ITELA

CHANGAMOTO kubwa kwa wahifadhi wa wanyama kwa sasa ni kuhakikisha wanyamapori wana mazingira bora na kumaliza mzozo kuhusu matumizi ya ardhi.

Wanadamu wanaendelea kupunguza makao ya wanyamapori kwa kuendeleza shughuli za kilimo na ujenzi. Jambo hili limeongeza visa vya mgogoro kati yao na wanyamapori. Visa hivi vinaashiria kukosekana kwa mfumo mzuri wa uhifadhi.

Uhifadhi wa maliasili uko katika njiapanda na kunahitajika hatua za dharura – serikali za kaunti na ya taifa – kuhakikisha kuna mazingira bora na uhusiano mwema wa wanadamu, mimea na Wanyama.

Kudunisha mazingira ni kudunisha maisha yetu. Tunategemea misitu na wanyama kwa chakula, dawa na mahitaji mengine ya msingi. Kwa hivyo, hali ya sasa ambapo ardhi inatumika visivyo, yafaa ikomeshwe.

Ili kuishi kwa utulivu na wanyamapori, inatupasa tuangazie jinsi ya kugawa ardhi na maliasili yake na muhimu zaidi, kuhakikisha wanyama wana eneo na mahitaji yao wakati wowote. Ruwaza yetu ya mwaka 2030 inatambua haja ya kuhakikisha kuna ushirikiano wa binadamu na wanyama, kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Kenya ina sera na sheria bora kuhusu usimamizi wa rasilimali, lakini tunaendelea kufeli katika uhifadhi kwa sababu hakuna ushirikiano.Pia kuna tatizo la utumizi wa ardhi ambapo hata hifadhi ya kibinafsi inapokuwa na mipango mizuri, hutakikana pia iwe na kanuni zinazowiana na za serikali husika za kaunti.

Ripoti ya majuzi kuhusu maeneo ya wanyamapori kupitia na kuishi, haijaanza kuetekelezwa.Maswali ambayo hayajajibiwa ni; eneo hilo litakuwa shambani mwa nani? Mwenye shamba alihusishwa kwenye mipango?

Ni upi mpango wa fidia? Mbuga za kitaifa kama Masai Mara, Nairobi National Park, Amboseli, Tsavo (Mashariki na Magharibi) na Aberdares haziwezi kustawi bila ya kuwepo mazingira bora.Bw Itera ni Afisa Mkuu Mtendaji wa Conservation Alliance of Kenya

You can share this post!

Mawaziri 4 wampuuza Naibu Rais

Miguna adai balozi alipuuza amri ya korti

T L