MUUNGANO wa Kenya Kwanza umeahidi kupiga marufuku matumizi ya mashine za kuchuma chai, endapo utashinda urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Akiendesha kampeni katika kaunti za Kericho na Bomet ambazo ni maarufu kwa kilimo cha majani chai, mgombea mwenza wa Naibu Rais William Ruto, Bw Rigathi Gachagua , alisema kuwa mashine hizo zimechangia kufutwa kazi kwa watu wengi.
Walilalama kuwa mashine moja hufanya kazi ambayo ingefanywa na zaidi ya watu 600 ambao sasa wanahangaika kwa kukatiziwa chanzo cha mapato.
Lakini Bw Gachagua na wenzake, wasije wakasahau kuwa mfumo wa uchumaji majani chai kwa mashine, ulianzishwa nchini kati ya miaka ya 2008 na 2009 wakati ambapo Dkt Ruto ndiye alikuwa Waziri wa Kilimo nchini.
Dkt Ruto hakupinga hatua ya kampuni kama vile Uniliver na Finlay kuleta mashine hizo humu nchini, na kuzindua matumizi yazo katika mashamba ya zao hilo katika kaunti za Kericho, Bomet na Nandi.