NA WANTO WARUI
HATIMAYE siku ya watahiniwa wa mitihani ya Darasa la Nane (KCPE) na Gredi ya Sita (KPSEA) kufanya mitihani hiyo imewadia.
Zaidi ya wanafunzi milioni tatu wataanza mitihani yao leo huku kukiwa na sintofahamu kuhusu mustakabali wa masomo ya CBC ambayo yamezua ubishi miongoni mwa washikadau wa elimu.
Jopo lililoundwa na Rais William Ruto kutathmini mfumo mzima wa elimu na kutoa mapendekezo yake linatarajiwa kuleta afueni kwa maelfu ya wazazi ambao wanalia kuhusu gharama ya masomo hayo ya CBC.
Katika kipindi hiki cha mitihani, ni vizuri kwanza watu waweke tofauti na mitazamo yao tofauti kando na wawape amani wanafunzi wote wanaofanya mitihani ili waweze kuafikia malengo yao ya elimu.
Tayari kuna baadhi ya wazazi wamesikika wakisema mtihani wa Gredi ya Sita, KPSEA, sio muhimu kama ule wa Darasa la Nane, KCPE.
Huku ni kudunisha wanafunzi hao na wakiachiliwa bila msaada au kuongozwa vizuri hawataweza kufikia malengo yao.
Pia, kuna shule nyingi ambazo zimekaribiana sana na maeneo ya starehe. Sehemu hizi hupooromosha muziki kwa sauti ya juu sana na hivyo kuvuruga masomo mara kwa mara. Serikali inapasa iwe macho na kuwasiliana na wasimamizi wa sehemu hizi za burudani ili kupunguza kelele au kuzifunga kabisa mitihani inapoendelea.
Hatua za kisheria zichukuliwe ikiwemo kunyanganya leseni wale hawatashirikiana. Kelele kama hizo bila shaka huwachanganya wanafunzi akili na wengine huishia kuandika yale yasiyofaa.
Aidha, baadhi ya wazazi hukabiliana kwa matusi na vita nyumbani mbele ya watoto. Wizi wa mtihani ni jambo jingine ambalo linaweza kuvuruga amani ya wanafunzi. Kila mwaka tunapata habari za wizi wa mitihani.
Serikali iweke mikakati bora kuhakikisha hili halitendeki.
Subscribe our newsletter to stay updated