• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:31 PM
Arsenal wachapa West Ham na kupepea zaidi kileleni mwa jedwali la EPL

Arsenal wachapa West Ham na kupepea zaidi kileleni mwa jedwali la EPL

Na MASHIRIKA

KOCHA Mikel Arteta amesema mkufunzi wa zamani wa Arsenal, Arsene Wenger, “aliteua wakati mwafaka zaidi” wa kurejea ugani Emirates kwa kuwa uwepo wake ulichochea kikosi hicho kuweka wazi azma ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu.

Kikosi kichanga cha Arsenal kilitoka nyuma kwa bao moja na kufunga West Ham mabao matatu ya haraka katika kipindi cha pili na kusajili ushindi wa 3-1 ugani Emirates.

Matokeo hayo yaliwezesha Arsenal kufungua mwanya wa alama saba kileleni mwa jedwali la EPL. Sasa wanajivunia pointi 40 huku nambari mbili Newcastle United wakiwa na alama 33, moja kuliko mabingwa watetezi Manchester City ambao wana mechi mbili zaidi za akiba.

Wenger ambaye ni kocha wa mwisho kushinda taji la EPL akidhibiti mikoba ya Arsenal, alirejea ugani Emirates kwa mara ya kwanza Jumatatu usiku tangu aagane na kikosi hicho mnamo 2018.

West Ham walifutiwa machozi na Said Benrahma aliyefunga penalti baada ya Jarrod Bowen kuchezewa visivyo na William Saliba ndani ya kijisanduku.

Mabao ya Arsenal yalifumwa wavuni kupitia Bukayo Saka, Gabriel Martinelli na Eddie Nketiah walioshirikiana vilivyo na nahodha Martin Odegaard.

West Ham wanaonolewa na kocha David Moyes sasa wanakamata nafasi ya 16 kwa alama 14 sawa na Everton waliopigwa na Wolves 2-1 ugani Goodison Park.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

MUME KIGONGO: Wanaume wenye kiwewe hatarini kuugua maradhi...

Mwangaza alikiuka Katiba mara 62, kamati yaambiwa

T L