• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 12:48 PM
Arsenal wacharaza Norwich City na kupunguzia kocha Arteta presha ya kutimuliwa

Arsenal wacharaza Norwich City na kupunguzia kocha Arteta presha ya kutimuliwa

Na MASHIRIKA

ARSENAL walimpunguzia kocha Mikel Arteta presha ya kupigwa kalamu baada ya kupepeta Norwich City 1-0 ugani Emirates na kusajili ushindi wao wa kwanza katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu.

Arteta alikuwa katika hatari ya kutimuliwa baada ya kikosi chake kupoteza mechi tatu za ufunguzi muhula huu wa 2021-22 dhidi ya Brentford, Chelsea na Manchester City mfululizo.

Pierre-Emerick Aubameyang alifungia Arsenal bao hilo la pekee na la ushindi katika dakika ya 66 baada ya mpira uliovurumishwa na Nicolas Pepe kugonga mhimili wa lango na kumbabatiza kipa Tim Krul.

Ilimjuzu refa Michael Oliver kurejelea teknolojia ya VAR kabla ya kuhesabu bao hilo la Arsenal.

Kati ya wanasoka wa Arsenal walioridhisha pakubwa katika gozi hilo ni sajili mpya Ben White aliyeshirikiana vilivyo na difenda Gabriel Magalhaes. Mchuano huo ulimpa Arsenal jukwaa mwafaka la kumwajibisha kipa Aaron Ramsdale aliyetokea Sheffield United muhula huu. Thomas Partey naye aliyepona jeraha aliletwa ugani katika kipindi cha pili kupiga jeki mashambulizi ya Arsenal ambao kwa sasa wanajivunia alama tatu kutokana na mechi nne zilizopita.

Arsenal wangalifunga mabao zaidi mwishoni mwa kipindi cha pili iwapo viungo wavamizi Emile Smith-Rowe na Bukayo Saka wangalitumia ipasavyo nafasi za wazi walizozipata.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO 

You can share this post!

Allan Wanga asema ‘tosha gari’ baada ya kutandaza soka...

Kampeni: Wabunge wako mbioni kubatilisha kanuni za IEBC