• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 10:50 AM
Allan Wanga asema ‘tosha gari’ baada ya kutandaza soka miaka 14

Allan Wanga asema ‘tosha gari’ baada ya kutandaza soka miaka 14

Na GEOFFREY ANENE

MSHAMBULIAJI Allan Wetende Wanga ametangaza kuangika daluga zake baada ya kucheza soka ya malipo katika klabu nane tofauti nchini Kenya, Angola, Azerbaijan, Vietnam, Sudan na Tanzania.

Wanga, 35, ambaye amemalizia taaluma yake Kakamega Homeboyz, alitoa tangazo hilo kupitia mitandao yake ya kijamii. Alisema kuwa kupitia soka ameweza kufika katika mataifa ambayo hakutarajia.

“Nimeonja ushindi na vichapo, kunyanyua makombe, kustahimili masikitiko ya kupokonywa ushindi kinywani na kutiwa moyo na jeshi la mashabiki kupitia upendo wao na usaidizi. Bila wewe, mashabiki wangu, wachezaji wenzangu, benchi za kiufundi za klabu nimechezea, familia yangu, sidhani kama ningekuwa na motisha ya kuendelea,” alisema na kutoa shukrani zake kwa waliochangia katika safari yake ya uchezaji.

“Shukran na Mungu akubariki. Tuonane nje ya uwanja,” alisema.

Klabu alizochezea Wanga ni Tusker, Sofapaka, AFC Leopards na Homeboyz (Kenya), Petro Luanda (Angola), FC Baku (Azerbaijan), Gia Lai (Vietnam), Al Merreikh (Sudan) na Azam (Tanzania). Alisakata zaidi ya mechi 160 humu nchini na kupachika karibu magoli 60.

Msimu wake mzuri nchini ulikuwa 2018-2019 alipotetemesha nyavu mara 18.

You can share this post!

Kampuni ya pembejeo kuzindua kiwanda cha kutengeneza mbolea...

Arsenal wacharaza Norwich City na kupunguzia kocha Arteta...