• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:57 PM
BB Erzurumspor yaendea kufufuka Uturuki tangu Omolo atue huko

BB Erzurumspor yaendea kufufuka Uturuki tangu Omolo atue huko

Na GEOFFREY ANENE

KLABU ya Buyuksehir Belediye Erzurumspor anayochezea Mkenya Johanna Omolo imetoka kwenye mduara wa kutemwa baada ya muda mrefu kufuatia ushindi wa 2-0 dhidi ya wenyeji Rizespor katika Ligi Kuu ya Uturuki, Ijumaa usiku.

Kiungo Omolo,31, alijiunga na timu hiyo ikivuta mkia Januari 14 akitokea Cercle Brugge kwenye Ligi Kuu ya Ubelgiji.

Timu hiyo maarufu kama BB Erzurumspor haijapoteza tangu awasili ikizoa ushindi dhidi ya Kasimpasa (2-1), Ankaragucu (1-0) na Rizespor na kuokota alama moja katika sare za 1-1 dhidi ya Alanyaspor na Kayseripor na kutoka 0-0 dhidi ya Sivasspor.

Ushindi ambao umefanya BB Erzurumspor kutoka katika mduara hatari na kukalia nafasi ya 15 kwenye ligi hiyo ya timu 21, ulipatikana kupitia mabao ya mshambuliaji Mmoroko Aatif Chahechouhe na nguvu-mpya Oltan Karakullukcu.

Omolo, ambaye ameshiriki mechi sita mfululizo, alipumzishwa dakika ya 72 na nafasi yake kutwaliwa na Rahman Cagiran.

Rizespor ilikamilisha mchuano huo watu 10 baada ya Mbrazil Fernando kuonyeshwa kadi nyekundu zikisalia dakika saba kipenga cha mwisho kilie.

You can share this post!

Yaya Toure arejea Ukraine kuwa kocha wa kikosi cha Olympic...

BI TAIFA FEBRUARI 13, 2021