• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:07 PM
Burnley wazidisha masaibu ya kocha Antonio Conte kambini mwa Spurs

Burnley wazidisha masaibu ya kocha Antonio Conte kambini mwa Spurs

Na MASHIRIKA

KOCHA wa Tottenham Hotspur, Antonio Conte, amefichua uwezekano wa kuagana na Tottenham Hotspur baada ya matumaini ya kikosi hicho kufuzu kwa soka ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu ujao kudidimia.

Ilikuwa mara ya kwanza kwa Burnley kushinda mechi mbili mfululizo za EPL chini ya kipindi cha miezi 13. Walishuka dimbani wakiwa na ari ya kuendeleza ubabe uliowavunia ushindi wa 3-0 dhidi ya Brighton katika mchuano wa awali ligini.

Chini ya Conte, Spurs waliduwazwa na Burnley kwa kichapo cha 1-0 mnamo Jumatano usiku ugani Turf Moor. Mechi hiyo ilikuwa ya nne kati ya tano zilizopita kwa Spurs kupoteza katika EPL.

Fowadi Ben Mee alifungia Burnley bao la pekee na ushindi katika mchuano huo uliowashuhudia wakipaa hadi nafasi ya 18 kwa alama 20, mbili mbele ya Watford na tatu zaidi kuliko Norwich City wanaovuta mkia.

Mwishoni mwa mechi, Conte, 52, alielekea moja kwa moja hadi chumba cha kubadilishia sare kabla ya kutoka nje kwa hasira.

“Nilikuja hapa kusaidia klabu na iwapo tatizo lao kubwa ni kocha au mbinu zangu za ukufunzi, basi niko tayari kubanduka. Hilo halina tatizo,” akasema.

“Sijazoea hali kama hizi za kushinda mechi muhimu na kupoteza nyingine ambayo kila mmoja alitarajia tushinde. Niko radhi kuzungumza na klabu kuhusu wanavyotaka ili tufanye kazi ya kuonekana. Ninajitahidi sana kwa ajili ya klabu hii,” akasisitiza mkufunzi huyo wa zamani wa Juventus, Chelsea na Inter Milan.

Hadi alipoaminiwa kuwa mrithi wa kocha Nuno Espirito Santo aliyetimuliwa na Spurs mnamo Novemba 2021, Conte amesimamia mechi 22 kambini mwa kikosi hicho ambacho sasa kinashikilia nafasi ya nane kwa alama 39, saba nyuma ya nambari nne Manchester United.

Hata hivyo, nafuu zaidi kwa Spurs wanaolenga kuwa miongoni mwa vikosi vitakavyokamilisha kampeni za EPL msimu huu ndani ya mduara wa nne-bora ni kwamba Man-United wametandaza mechi mbili zaidi kuliko 24 ambazo wao wamesakata.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Liverpool waponda Leeds United na kuendeleza presha kwa...

Miradi ya handisheki yakimbizwa ikamilike

T L