• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 6:50 AM
Chelsea warefusha mkia wa Norwich City ligini

Chelsea warefusha mkia wa Norwich City ligini

Na MASHIRIKA

CHELSEA walizidisha masaibu ya Norwich City katika kampeni za Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu kwa kuwatandika 3-1 mnamo Alhamisi usiku ugani Carrow Road.

Mashabiki wa Chelsea waliokuwa wamesafiri kuhudhuria mechi hiyo waliimba wimbo wa Roman Abramovich wakati wa vipindi vyote viwili vya mchezo huo baada ya bwanyenye huyo raia wa Urusi kuwekewa vikwazo na kupigwa marufuku na Uingereza kutokana na ushambulizi unaotekelezwa na taifa lake la Urusi dhidi ya Ukraine.

Chelsea iliyoanzishwa miaka 117 iliyopita, ilichukua uongozi wa mabao 2-0 katika dakika 15 za ufunguzi wa kipindi cha kwanza na wakaishia kusajili ushindi wan ne mfululizo ligini.

Trevoh Chalobah alifungulia Chelsea ukurasa wa mabao katika dakika ya tatu baada ya kushirikiana vilivyo na fowadi Mason Mount. Kai Havertz alichangia bao la pili ambalo Chelsea walifungiwa na Mount. Kiungo huyo mvamizi raia wa Uingereza sasa anajivunia mabao manane msimu huu.

Ushindi wa Chelsea uliwadumisha katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa jedwali kwa alama 56, nane zaidi kuliko Arsenal wanaofunga orodha ya nne-bora.

Zikisalia mechi 10 pekee kwa kampeni za EPL msimu huu kutamatika rasmi, Norwich kwa sasa wanavuta mkia wa jedwali kwa alama 17 kutokana na mechi 28.

Mbali na mchuano dhidi ya Burnley ambao pia wako katika hatari ya kuteremshwa ngazi ligini msimu huu, Norwich wangali na kibarua kigumu dhidi ya West Ham United (nyumbani), Tottenham (nyumbani) na Manchester United (ugenini) ambao wanafukuzia fursa ya kumaliza kampeni za msimu huu ndani ya orodha ya nne-bora.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

‘Polisi walioitisha hongo kwa sababu ya barakoa...

Uingereza yavuruga mpango wa Abramovich kuuza Chelsea

T L