Chepng’etich na Kipruto mibabe Chicago Marathon
Na GEOFFREY ANENE
NYOTA Ruth Chepng’etich aliibuka malkia mpya wa Chicago Marathon baada ya kuongoza mbio hizo kutoka mwanzo hadi mwisho nchini Amerika jana Jumatatu.
Dakika chache baada ya Mkenya mwenzake na bingwa wa Boston Marathon Benson Kipruto kutawala kitengo cha wanaume kwa saa 2:04:24, bingwa wa dunia 2019 Chepng’etich alikosa rekodi ya dunia kwa sekunde 14 akinyakua taji kwa 2:14:18.
Chepng’etich kutoka Idara ya Magereza alikuwa ndani ya rekodi ya dunia kwa kipindi chote, lakini akaipoteza.
Chepng’etich aliingia kilomita mbili za mwisho akiwa sekunde nne ndani ya rekodi ya dunia ya Mkenya Brigid Kosgei (2:14:04).
Hata hivyo, Chepng’etich alifanikiwa kuweka muda wake mpya bora 2:14:18 kutoka 2:17:08 aliokuwa ametimka akitawala Dubai Marathon 2019. Ni matokeo mazuri ya Chepng’etich, hasa ikilinganishwa kuwa alikosa kumaliza Olimpiki 2020 mjini Tokyo, Japan na pia Riadha za Dunia miezi mitatu iliyopita jimboni Oregon, Amerika.
Emily Sisson jana alikamata nafasi ya pili kwa rekodi mpya ya Amerika 2:18:29 baada ya kufuta ya Keira D’Amato (2:19:12) iliyowekwa Januari 16 mjini Houston. Vivian Kiplagat alifunga tatu-bora (2:20:52).
Kipruto, ambaye alishinda Boston Marathon 2021, alikuwa amepigiwa upatu kutawala na hakusikitisha. Alichukua uongozi kabisa zikisalia kilomita mbili. Alifuatiwa kwa karibu na Muethiopia Seifu Tura (2:04:49) na Wakenya John Korir (2:05:01) na Bernard Koech (2:07:15).
Tuzo
Nafasi tano za kwanza ziliandamana na tuzo ya Sh9.1 milioni, Sh6.6m, Sh5.4m, Sh3.6m na Sh3.0m mtawalia.
Chepng’etich alikosa pembemba Sh9.1m bonasi ya kuweka rekodi ya Chicago Marathon. Katika mbio zingine zilizofanyika Jumatatu, Bornes Kitur alitwaa umalkia wa Lisbon Marathon nchini Ureno kwa saa 2:24:17 akiwa ni Mkenya wa kwanza kufanya hivyo tangu Sarah Chepchirchir mwaka 2017.
Agnes Keino (2:23:26) na Philimon Kipchumba (2:07:28) walitawala Munich Marathon nchini Ujerumani wakiwa ni Wakenya wa kwanza kupata ufanisi huo tangu Michael Kite mwaka 2000.
Hildah Jepkosgei aliibuka mshindi katika Sofia Marathon kwa 2:45:52 nchini Bulgaria naye Naaman Serem akakamata nafasi ya pili (2:18:04). Pius Karanja (2:06:55) aliongoza Gevin Kerich (2:07:07) na Joshua Kemboi (2:08:09) kufagia nafasi tatu za kwanza Eindhoven Marathon nchini Uholanzi naye Paskalia Chepkosgei (2:22:47) akashinda kitengo cha kinadada.
Next article
Afisa ashauri wakazi kuwekeza kwa ufugaji samaki ili...