Commander Okoth atinga nusu-fainali ya ndondi za Urusi
Na AYUMBA AYODI
Mkenya Nick “Commander” Okoth ameingia nusu-fainali ya mashindano ya masumbwi ya makumbusho ya Konstantin Kototkov mjini Khabarovsk, Urusi.
Okoth alizoa ushindi kwa wingi pointi dhidi ya Sergey Kishko kutoka Ukraine katika uzani wa unyoya mnamo Alhamisi. Majaji wote watano walimpa Okoth ushindi wa alama 29-28, 30-27, 30-27, 30-27 na 30-27.
Okoth sasa atalimana na mwenyeji Ovik Oganisyan kutafuta tiketi ya fainali hapo Ijumaa, huku Mkenya mwingine Elly Ajowi akipepetana na Mamadiyar Saydrahimov kutoka Uzbekistan katika robo-fainali ya uzani wa “Super heavy”.
Ushindi wa Okoth ulipatikana muda mchache baada ya mshindi wa nishani ya shaba ya Jumuiya ya Madola, Christine Ongare na bingwa wa taifa wa uzani wa “bantam” Elizabeth Akinyi kubanduliwa katika raundi ya kwanza ya vitengo vyao.
Ongare alishindwa kwa wingi wa alama na Diana Garishnaya kutoka Estonia naye Akinyi akaambulia kichapo sawa na hicho dhidi ya Maria Moronto kutoka Jamhuri ya Dominican.
Shirikisho la Ndondi zisizo za malipo duniani (AIBA) linatumia mashindano hayo kuandaa mabondia waliofuzu kushiriki michezo ya Olimpiki mjini Tokyo nchini Japan.
Serikali na Kamati ya Kitaifa ya Olimpiki Kenya (NOC-K) wamefanikisha ziara ya kikosi cha mchezo wa ngumi cha Kenya maarufu kama Hit Squad.
Next article
Rangers yalenga rekodi ya kukamilisha msimu bila kulimwa