Na GEOFFREY ANENE
MKENYA McRae Kimathi amekamilisha mkondo wa sita wa duru ya Mbio za Magari Duniani (WRC) ya Ureno katika nafasi ya nne katika kitengo cha chipukizi Mei 20.
Dereva huyo mwenye umri wa miaka 27, ambaye anaelekezwa na Muingereza Stuart Loudon baada ya kuweka pembeni Mkenya mwenzake Mwangi Kioni, yuko dakika mbili na sekunde 20.2 nyuma ya Sami Pajari kutoka Finland anayeongoza kwa dakika 14:57.1.
Muingereza Jon Armstrong anakamata nafasi ya pili sekunde 17.5 nyuma ya Pajari naye Lauri Joona kutoka Finland anakamilisha tatu-bora sekunde 41.3 nyuma.
Kimathi, ambaye anaendesha gari la Ford Fiesta R3, yuko mbele ya William Creighton kutoka Ireland na Robert Virves kutoka Estonia walio dakika 5:26.0 na 12:01.9 nyuma.
Bingwa huyo wa Afrika kitengo cha chipukizi alikamata nafasi ya sita katika mikondo ya kwanza, tatu, nne na sita na nambari nne katika mikondo ya pili na sita.
Nafasi tatu za kwanza katika mashindano kwa jumla zinakaliwa na Elfyn Evans kutoka Wales, raia wa Finland Kalle Rovanpera na Mhispania Dani Sordo.