Na MASHIRIKA
JIJI la Istanbul nchini Uturuki litakuwa mwenyeji wa fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo 2023 huku fainali ya Europa League ikifanyika jijini Dublin, Jamhuri ya Ireland.
Istanbul ambalo ni jiji kuu la Uturuki linachukua nafasi ya Munich, Ujerumani baada ya fainali ya UEFA 2021 kuhamishwa kutoka Istanbul hadi Porto nchini Ureno.
Ukali wa kanuni za kudhibiti maambukizi ya corona ulishuhudia fainali ya UEFA mnamo Mei 2021 ikitolewa uwanjani Ataturk Olympic nchini Uturuki siku 16 kabla ya Chelsea walioibuka mabingwa kushuka dimbani kuvaana na Manchester City.
Dublin imepata fursa ya kuandaa fainali ya Europa League uwanjani Aviva baada ya mechi nne za kipute cha Euro mwaka huu kuhamishwa kutoka jiji hilo.
Jiji la Lisbon nchini Ureno lilitwikwa jukumu la kuwa mwenyeji wa kipute cha UEFA mnamo 2019-20 kuanzia hatua ya nane-bora. Bayern Munich ya Ujerumani walishinda Paris Saint-Germain (PSG) ya Ufaransa 1-0 na kutwaa ufalme wa msimu huo.
Kwa mujibu wa mabadiliko ya sasa, uwanja wa Allianz Arena jijini Munich sasa utatumiwa kuandalia fainali ya UEFA mnamo 2025 badala ya 2023.
Fainali ya UEFA mnamo 2024 itasalia katika uwanja wa Wembley jijini London, Uingereza huku fainali ya mwaka ujao wa 2022 ikitarajiwa kufanyika jijini St Petersburg, Urusi.
Fainali ya Europa League mnamo 2025 itafanyika jijini Bilbao, Uhispania. Jiji hilo litaandaa pia fainali ya UEFA kwa wanawake mnamo 2024.
MWAKA | UEFA | EUROPA LEAGUE |
2022 | St Petersburg, Urusi | Seville, Uhispania |
2023 | Istanbul, Uturuki | Budapest, Hungary |
2024 | Wembley, London, Uingereza | Dublin, Jamhuri ya Ireland |
2025 | Munich, Ujerumani | Bilbao, Uhispania |
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO