• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 5:50 AM
FIFA yaidhinisha vikosi vya masogora 26 kwa ajili ya Kombe la Dunia 2022

FIFA yaidhinisha vikosi vya masogora 26 kwa ajili ya Kombe la Dunia 2022

Na MASHIRIKA

SHIRIKISHO la Soka Duniani (FIFA) limeidhinisha ombi la washiriki wa Kombe la Dunia mwaka huu nchini Qatar kutaja vikosi vya wachezaji 26.

Hatua hiyo ni upanuzi wa vikosi vya wanasoka 23 vilivyokuwa vikitumika hapo awali kabla ya janga la corona.

Kwa mujibu wa FIFA, hadi wachezaji 15 wa akiba wanaweza kutajwa kwenye mchuano mmoja, kumaanisha hakuna sogora atakayekosa nafasi ya kuhusishwa katika mechi – jambo ambalo kocha wa Uingereza, Gareth Southgate amekuwa akilisukuma sana.

“Ni vyema kwa kila mchezaji kuhusika katika mechi. Ikiwa vikosi vitapanuka, basi mpango huo utampa kila mchezaji fursa ya kuchangia matokeo ya kikosi chake siku ya mchuano,” akasema Southgate.

Makataa kwa mataifa yote 32 yatakayonogesha fainali zijazo za Kombe la Dunia kuwasilisha vikosi vyao vya mwisho kwa FIFA ni Oktoba 20, siku 30 kabla ya Senegal na Uholanzi kufungua fainali hizo kwa pambano litakalofanyika ugani Al Thumama.

FIFA imesisitiza kuwa watu wasiozidi 26 – hadi wachezaji 15 wa akiba na maafisa 11 wa timu, ambapo mmoja wao lazima awe daktari wa timu – wataruhusiwa kukaa kwenye benchi.

Uingereza watafungua kampeni zao za Kundi B dhidi ya Iran mnamo Novemba 21 kabla ya Wales kupimana ubabe na Amerika. Bara la Afrika linawakilishwa na Ghana, Tunisia, Morocco, Cameroon na Senegal ambao ni wafalme wa Kombe la Afrika (AFCON).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO 

  • Tags

You can share this post!

Man-City wang’oa Kalvin Phillips kambini mwa Leeds...

PENZI LA KIJANJA: Kuepuka uvundo wa upweke!

T L