IMEKUSANYWA NA CECIL ODONGO
KOCHA Brendan Rodgers amesema kuwa nyota wake Wesley Fofana ametulia na kumakinikia kuchapa shughuli msimu huu baada ya Leicester City kukataa mara mbili ofa ya Chelsea.
Beki huyo mwenye umri wa miaka 21 amekuwa akiwindwa na Kocha Thomas Tuchel lakini Leicester City imekataa mara mbili ofa za Sh9.1 bilioni na Sh10.1 bilioni mtawalia.
Fofana, raia wa Ufaransa alitia saini mkataba wa muda mrefu wa kusalia ugani King Power mnamo Machi, inadaiwa ameridhia kusalia Leicester City na haonekani kumakinikia kuelekea Chelsea.
Japo Chelsea huenda wakawasilisha ofa ya tatu, Rodgers anasema Leicester City haiko tayari kumuuza na pesa ambazo Chelsea imeleta za kumnunua mwanadimba huyo ni kidogo sana.