Na GEOFFREY ANENE
Kenya hatimaye imepata medali yake ya kwanza ya dhahabu kwenye Olimpiki 2020 baada ya Emmanuel Korir na Ferguson Rotich kufagia nafasi mbili za mbio za mita 800 jijini Tokyo, Japan mnamo Agosti 4.
Mkazi wa Amerika Korir, ambaye alionyeshwa kadi nyekundu katika mbio za mchujo za mita 400 siku chache zilizopita, alipata kitulizo aliposhinda mizunguko hiyo miwili kwa dakika 1:45.06. Alipata medali hiyo yake ya kwanza kubwa baada ya kuchukua uongozi katika mita 150 za mwisho.
Rotich alimpita Patryk Dobek kutoka Poland zikisalia chini ya mita 50 baada ya kutoka karibu nafasi ya tano. Dobek aliridhika na shaba kwa dakika 1:45.39 naye Rotich alimaliza na 1:45.23.
Bingwa wa zamani wa dunia Nijel Amos, ambaye alikuwa amepigiwa upatu kung’ara, alimaliza katika nafasi nane kati ya washiriki tisa. Rotich alimaliza nafasi ya tano kwenye Olimpiki 2016 nchini Brazil.
Medali za Korir na Rotich zilipatikana dakika chache baada ya bingwa wa dunia mbio za mita 3,000 kuruka viunzi na maji Hyvin Kiyeng kushindia Kenya nishani ya shaba katika kitengo hicho cha kinadada.