Na JOHN KIMWERE
MECHI mbili zimepangwa kuchezwa (Alhamisi) kwenye mfululizo wa kampeni za kuwania taji la Koth Biro ambapo ni makala ya 43.
Ngara Youth itaingia mzigoni kucheza Rongai United nao wanasoka wa Biafra Kamaliza watakutanishwa na Macmillan FC ugani Umeme Ziwani, Nairobi. Kwenye matokeo ya mechi za utangulizi, Wilson Muzungu alicheka na wavu mara moja na kuibeba Wenyeji Youth kuzaba Wayaba FC bao 1-0.
Nayo Kisima FC ilitoka sare tasa dhidi ya Camchedus kwenye mechi za Kundi A. Shindano hilo limekuwa likiandaliwa kila mwaka wakati wa mvua na huvutia wachezaji wengi tu kutoka timu mbali mbali katika Kaunti ya Nairobi.
Kwa mara ya kwanza kiongozi wa chama cha ODM, Raila Odinga atadhamini shindano la mwaka huu. Mashindano ya mwaka huu yamevutia timu 46 ambazo zimegwanywa kwa makundi manne. Raila ndiye aliyezindua mechi za kinyang’anyiro cha mwaka huu.
Kiongozi aliahidi kuwa uwanja huo utafanyiwa ukarabati. ”Michezo ni muhimu hasa soka ambayo imefanya wachezaji wengi matajiri. Uwanja wa Umeme umetoa wachezaji wengi waliobahatika kuchezea klabu tofauti nchini pia nchi za kigeni bila kusahau timu ya Harambee Stars,” Raila alisema.
Dallas Allstars ndiyo mabingwa watetezi baada ya kushinda Ruaraka Akllstars kwa mabao 8-7 kupitia mipigo ya matuta baada ya kutoka sare tasa katika muda wa kawaida mwaka jana. Mshindi wa kipute cha mwaka huu atapokea zawadi ya Sh300, nambari mbili atatuzwa Sh100,000, nambari tatu na nne watapongezwa kwa Sh 50,000 na Sh20,000 mtawalia.