Mechi hiyo ya Ligi Kuu ya Wanawake nchini (KWPL) ya raundi ya 14, ilisakatwa ugani Camp Toyoyo jijini Nairobi.
Kiungo Diana Wachera alicheka na wavu wa kwanza mapema dakika ya pili. Ann Arusi aliongezea bao la pili dakika ya 15 nae Elizabeth Wambui akafunga shughuli ya siku dakika za lala salama kipindi cha pili.
Ugani GEMS Cambridge kaunti ya Kajiado, bao la mshambulizi Maureen Ater dakika ya 62 dhidi ya Zetech Sparks, lilitosha kuwafanya Vihiga Queens kuendelea kupambania taji la ligi.
Vihiga walishuka hadi nafasi ya pili na alama sawa na Gaspo lakini wanatofautiana na mabao. Kufikia sasa Gaspo na Vihiga na bao moja wana jumla ya mabao 37 na 36 mtawalia.
Kulingana na kocha wa Vihiga Boniface Nyamunyuma, ushindani mkali kwenye ligi unachangia wao kujituma zaidi uwanjani.
“Ilikuwa mechi ngumu ikilinganishwa kwamba ligi pia inaushindani mkali na kila timu inataka kushinda. Hizi alama tatu ni muhimu kwetu, zitatupa morale tunaporejea nyumbani kujiandaa kwa mechi ifuatayo,” alisema Nyamunyamu.
Kwa upande wa kocha msaidi wa Zetech Jackson Tumaini, ambaye alivalia viatu vya kocha mkuu Bernard Kitolo kwenye mechi hiyo, anasema walilegeza kamba kwenye mashambulizi.
“Tulikuwa na nafasi nyingi za wazi za kufunga haswaa katika kipindi cha pili lakini hatukufanikiwa kufunga. Hayo yamepita sasa tunajiandaa kwa mechi ifuatayo ya ligi,” alisema Tumaini.