• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 6:40 PM
KWPL: Mabingwa Vihiga Queens wakamilisha msimu kwa kutandika Gaspo Women 2-1

KWPL: Mabingwa Vihiga Queens wakamilisha msimu kwa kutandika Gaspo Women 2-1

NA TOTO AREGE

VIHIGA Queens wameshinda Gaspo Women 2-1 na kutangazwa mabingwa wa Ligi Kuu ya Wanawake ya Kenya (KWPL) msimu wa 2022/23 kwenye mechi ya mzunguko wa mwisho wa msimu.

Mechi hiyo iliyosakatwa katika uwanja mpya wa Police Sacco jijini Nairobi, haikuwa mechi ya lazima kwa Vihiga kushinda kwa sababu, tayari walikuwa wametangazwa mabingwa baada ya ushindi wao wa 2-1 dhidi ya Nakuru City Queens wikendi iliyopita.

Wenyeji walipata bao la kuongoza dakika ya 20 kupitia kwa Adrian Birungi aliyechanja bao kwa kichwa kupitia kona iliyochongwa na kiungo Elizabeth Mutukiza.

Vihiga wangeweza kupata bao la kusawazisha dakika ya 34, lakini mpira wa kona uliopigwa na Bertha Omitta haukuzaa matunda kwani uliishia kugonga mwamba wa goli baada ya Janet Moraa Bundi kuupiga kwa kichwa.

Bundi alifunga goli dakika ya 38 na lingine dakika 67 na kuhakikishia timu yake pointi tatu.

Gaspo walitumia kurasa zao za mitandao ya kijamii Ijumaa kuthibitisha kwamba walikuwa tayari kucheza mechi hiyo baada ya Jumatano wiki hii kutangaza kwamba hawangecheza dhidi ya Vihiga.

Kocha wa makipa wa Gaspo James Ombeng anasema msimu umekuwa na ushindani mkubwa.

“Tuliteleza kutwaa ubingwa tulipotoka sare mechi mbili mfululizo. Tumejifunza kutokana na makosa yetu na tutakuwa makini zaidi msimu ujao. Tutarejea kwa nguvu zaidi,” amesema Ombeng.

Kocha mkuu wa Vihiga Queens Boniface Nyamunyamuh amesema kwamba kila kitu kimetokea kulingana na mipango yao.

“Tumeshinda taji na ndilo tulilokuwa tukilifuata. Kushinda ligi hakumaanishi kuwa tulikuwa wakamilifu kwa sababu tulikuwa na pandashuka zetu,” amesema Nyamunyamuh.

Vihiga wamemaliza kileleni mwa jedwali wakiwa na alama 55 huku Gaspo wakiwa na alama 49.

Rais wa Shirikisho la Soka la Kenya (FKF) Nick Mwendwa alikabidhi Vihiga kombe naye makamu wake Doris Petra akawakabidhi hundi ya Sh1 milioni.

Katika uwanja huo huo, mabingwa wa zamani Thika Queens wameilaza Zetech Sparks 1-0 na kumaliza msimu kwa kishindo. Bao hilo la pekee limefungwa na Grace Wekesa.

Kisumu All Starlets wamelaza Trans Nzoia Falcons 6-0 katika uwanja wa Moi jijini Kisumu. Beth Achieng, Beverline Adika na Faith Ogeda walifunga mabao mawili kila mmoja. Hata baada ya ushindi huo, Kisumu imeshushwa daraja rasmi kutoka kwa ligi pamoja na Kangemi Ladies na Kayole Starlets.

Katika mechi nyingine iliyochezwa katika uwanja wa Mumboha ulioko Kaunti ya Vihiga, penalti ya Airin Madalina dakika ya 54 wakicheza dhidi ya Nakuru City Queens imetosha kuwaokoa Bunyore Starlets wasishuke daraja.

Madalina sasa ndiye mfungaji bora wa ligi akiwa na mabao 18 mbele ya mshambuliaji wa Thika Queens, Wendy Atieno.

  • Tags

You can share this post!

Panyako ajiuzulu nafasi yake ya Naibu Mwenyekiti UDA

Sipiganii tumbo langu, ninatetea mahasla – Raila

T L