Na MASHIRIKA
MADRID, Uhispania
KOCHA Jurgen Klopp amesema vijana wake wa Liverpool waliwapa “kazi rahisi” Real Madrid katika mechi ya mkondo wa kwanza ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA), mnamo Jumanne usiku.
Liverpool walilimwa 3-1 na vigogo hao wa Uhispania, katika uwanja wa Alfredo Di Stefano.
“Hatukuwa na mchezo mzuri wa kutatiza Real Madrid. Tulifanya mambo kuwa rahisi sana kwao. Tunachoweza kujiliwaza nacho ni kwamba mkondo ulikuwa wa kwanza. Hatukustahili chochote kutokana na mechi lakini bao hilo moja (la ugenini) litatufaa,” Klopp alisema baada ya mechi.
“Tuliwapa nafasi kubwa ya kutawala uwanjani, lakini tuko na fursa ya kulipiza kisasi.
“Itabidi tupigane vikali iwapo tunataka kutinga hatua ya nusu-fainali. Tukicheza jinsi tulivyocheza tutajilaumu kwa mara nyingine,” aliongeza kocha huyo Mjerumani.
Liverpool, almaarufu The Reds, watakuwa na kibarua kigumu kubatilisha matokeo hayo nyumbani Anfield, wakati wa mechi ya marudiano wiki inayokuja.
Walilemewa kabisa katika kipindi cha kwanza huku mabao ya Vinicius Junior (mawili) na Marco Asensio yakiwapa tabasamu masogora wa kocha Zinedine Zidane.
Fowadi Mohamed Salah alifungia Liverpool bao hilo la kufutia machozi.
Kocha Zidane, hata hivyo, amehimiza vijana wake kuwa chonjo akisema wangali na kazi ngumu mbele yao.
“Liverpool ni timu kubwa iliyo na uwezo wa kubadilisha matokeo haya tutakaporudiana Aprili 14,” alieleza Mfaransa huyo ambaye zamani alikuwa kiungo wa Real.
Kikosi chake kilikaa imara na kuzima matumaini yoyote ya Liverpool kujiongezea mabao ya ugenini.