Na GEOFFREY ANENE
KENYA imepoteza ubingwa wa London Marathon wa kitengo cha akina dada na utawala wa miaka sita baada ya Muethiopia Yalemzerf Yehualaw kubeba taji kwa saa 2:17:25 mjini London, Uingereza, Jumapili.
Bingwa mtetezi Joyciline Jepkosgei ameridhika na nafasi ya pili kwa 2:18:07 akifuatiwa na Alemu Megertu kutoka Ethiopia (2:18:32), mshindi wa nishani ya fedha ya Riadha za Dunia Judith Korir kutoka Kenya (2:18:43), Mromania Joan Chelimo (2:19:27), Muethiopia Ashete Bekere (2:19:30) na Mkenya Mary Wacera (2:20:22) mtawalia.
Yehualaw alichomoka hatua chache baada ya kufika katika kilomita ya 37 akiwa bega kwa bega na Jepkosgei ambaye alikosa jibu.
Kabla ya makala haya ya 42, Kenya ilikuwa imetawala makala sita mfululizo ya London Marathon katika kitengo cha wanawake kupitia kwa Jemima Sumgong (2016), Mary Keitany (2017), Vivian Cheruiyot (2018), Brigid Kosgei (2019 & 2020) na Jepkosgei (2021).
Mstaafu Keitany anashikilia rekodi ya dunia ya wanawake pekee ya 2:17:01 aliyoweka mwaka 2017.