• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
Mamilioni yatakayotumiwa na serikali kwenye mbio za Kip Keino Classic

Mamilioni yatakayotumiwa na serikali kwenye mbio za Kip Keino Classic

Na AYUMBA AYODI

Serikali itatumia Sh250 milioni kuhakikisha makala ya pili duru ya Riadha za Dunia za Continental Tour ya Kip Keino Classic yanakuwa ya kufana ugani Kasarani.

Katibu katika Wizara ya Michezo, Joe Okudo alisema hayo jana akikaribisha wanariadha 265 na maafisa watakaowania mataji Septemba 18.

Baadhi ya nyota wa kigeni wanaokuja ni Soufiane El Bakkali (Morocco), Peruth Chemutai (Uganda), Justin Gatlin (Amerika), Christine Mboma (Namibia), Isaac Makwala (Botswana) na Sinesipho Dambile (Afrika Kusini).

Aidha, rais wa Shirikisho la Riadha Kenya (AK) Jack Tuwei amefichua kutoka idadi ya washiriki 265, wanariadha 185 watashiriki mashindano ya washiriki wote na waliosalia yale yaliyotengewa watu maalum ugani Kasarani.

Tuwei alisema kuwa AK imealika wanariadha 80 wa humu nchini kushiriki mashindano ya kitaifa ya makala hayo ya pili yaliyohamishwa kutoka uwanja wa Nyayo hadi Kasarani kwa lengo la kuwapa washiriki vifaa bora zaidi.

Alisema kuwa maandalizi ya mashindano hayo ya siku moja yanakaribia kukamilika na yatazinduliwa rasmi Septemba 13 katika hoteli ya Ole Sereni jijini Nairobi.

Afisa huyo pia alifichua kuwa kwa mwaka wa pili mfululizo, mashabiki hawataruhusiwa uwanjani kutokana na masharti ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Covid-19.

Baadhi ya majina makubwa ya humu nchini yatakayoshiriki ni pamoja na bingwa wa Olimpiki Faith Chepng’etich (mbio za mita 1,500), mshindi wa medali ya fedha ya Olimpiki Ferguson Rotich (mita 800) na mshikilizi wa rekodi ya kitaifa ya mbio za mita 100 Ferdinand Omanyala.

TAFSIRI: GEOFFREY ANENE

You can share this post!

Uganda yaalika Rwanda uhusiano kati yao ukidorora

Wilbaro, Chungwa vyazua mabishano