• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
Matarajio makubwa ya mashabiki kutoka kwa Chelsea yanatutia presha – Tuchel

Matarajio makubwa ya mashabiki kutoka kwa Chelsea yanatutia presha – Tuchel

Na MASHIRIKA

KOCHA Thomas Tuchel wa Chelsea anatarajia beki Reece James kukosa mechi za timu ya taifa ya Uingereza kwa sababu ya jeraha.

Mnamo Septemba 30, 2021, James alijumuishwa katika kikosi kilichotajwa na kocha wa Uingereza, Gareth Southgate kwa minajili ya michuano ijayo ya kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2022 dhidi ya Andorra na Hungary.

Hata hivyo, Tuchel amesema maamuzi ya kujumuishwa kwa James, 21, kwenye kikosi hicho cha Uingereza ni “kosa la kutoeleweka kwa baadhi ya mambo.”“Nilishangaa sana kuona kwamba James ameitwa kambini mwa Uingereza.

Kwa sasa anauguza jeraha. Anashiriki mazoezi mepesi sana na sidhani atakuwa sehemu ya kikosi hicho cha Southgate.” Kulingana na uelewa wangu baada ya habari za hivi karibuni zaidi kutoka kwa madaktari wake, James hataungana na wenzake kambini mwa Uingereza.

Hivyo kuitwa kwake huenda kulichangiwa na kutoeleweka kwa baadhi ya mambo. Si chochote kingine,” akaongeza Tuchel. Aidha, mkufunzi huyo raia wa Ujerumani amesema kwamba ukubwa wa kiwango cha matarajio ya mashabiki kutoka kwa kikosi chake pia umeathiri uthabiti wa masogora wake kisaikolojia baada ya kikosi chake kupoteza mechi mbili mfululizo.

Chelsea walipigwa 1-0 na Juventus katika Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Septemba 29, 2021 baada ya kupokezwa kichapo sawa na hicho na mabingwa watetezi Manchester City katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mnamo Septemba 25, 2021 ugani Stamford Bridge.

Chelsea ambao ni mabingwa watetezi wa UEFA, watashuka dimbani mnamo Oktoba 2, 2021 kumenyana na Southampton katika EPL huku baadhi ya wachanganuzi wa soka wakiwapigia upatu wa kutwaa ufalme wa kivumbi hicho muhula huu.

“Sielewi kiini cha Chelsea kuwekwa mbele katika orodha ya wawaniaji halisi wa taji la EPL. Hilo linatutia presha bure. Kikosi kinaathirika zaidi kisaikolojia kinapopoteza mechi.

Ushindani ni mkali na hatuwezi kumbeza yeyote,” akasema kocha huyo wa zamani wa Paris Saint-Germain (PSG) na Borussia Dortmund.

  • Tags

You can share this post!

Rashford arejelea mazoezi baada ya kufanyiwa upasuaji...

Pep Guardiola akiri kwamba Jurgen Klopp amemfanya kuwa...