Na MASHIRIKA
KYLIAN Mbappe aliongoza Paris Saint-Germain (PSG) kusajili ushindi wa 2-1 dhidi ya Strasbourg katika Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1) mnamo Jumatano usiku.
Mechi hiyo ilikuwa ya kwanza kwa Mbappe kusakata tangu awe sehemu ya kikosi kilichowakilisha Ufaransa kwenye fainali ya Kombe la Dunia dhidi ya Argentina nchini Qatar mnamo Disemba 18, 2022.
Marquinhos aliwafungulia PSG ukurasa wa mabao katika dakika ya 14 kabla ya kujifunga na kusawazisha mambo mwanzoni mwa kipindi cha pili. PSG walikamilisha mchuano huo na wachezaji 10 pekee uwanjani baada ya fowadi Neymar Jr kuonyeshwa kadi nyekundu katika dakika ya 62.
Mbappe aliokoa jahazi ya PSG alipofunga mkwaju wa penalti sekunde chache kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mchezo kupulizwa. Penalti hiyo ilitokana na tukio la Mbappe kuchezewa visivyo na Gerzino Nyamsi ndani ya kijisanduku.
Ushindi huo ulidumisha PSG kileleni mwa jedwali la Ligue 1 kwa alama 44, nane zaidi kuliko nambari mbili Lens. Strasbourg kwa upande wao wanakamata nafasi ya 19 kwa pointi 11, tatu mbele ya Angers wanaovuta mkia.
MATOKEO YA LIGUE 1 (Jumatano):
PSG 2-1 Strasbourg
Ajaccio 1-0 Angers
Troyes 0-0 Nantes
Auxerre 2-3 Monaco
Clermont 0-2 Lille
Crest 2-4 Lyon
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO