Na GEOFFREY ANENE
MKENYA Dominic Ondoro ndiye mshindi wa Houston Marathon nchini Amerika.
Ondoro alikata utepe katika mbio hizo za kilomita 42 kwa saa 2:10:36 na kujizolea Sh4.3 milioni.
Ondoro, ambaye sasa ana mataji mawili ya Houston Marathon baada ya kutawala mwaka 2017, alifuatiwa na Muethiopia Ayana Tsedat (2:10:37) na Muamerika Teshome Mekonen (2:11:05) waliotia mfukoni Sh2.0 milioni na Sh864,033 mtawalia.
Hitomi Niiya kutoka Japan alitawala kitengo cha kinadada kwa muda wake bora wa saa 2:19:24 akifuatiwa na Waethiopia Muliye Dekebo (2:25:35) na Sintayehu Lewetegn (2:26:33).
Mkenya Wesley aliridhika na nafasi ya pili katika kitengo cha kilomita 21, akiandikisha muda wake bora wa 1:00:35, katikati ya mshindi Leul Gebresilase kutoka Ethiopia (1:00:34) na nambari tatu Mmoroko Mohamed El-Aaraby (1:00:58). Muethiopia Hiwot Gebrekidan (1:06:28), Muamerika Emily Sisson (1:06:52) na Muingereza Jess Warner-Judd walikamata nafasi tatu za kwanza katika kilomita 21 upande wa kinadada. Nafasi tatu za kwanza katika nusu-marathon zilizawadiwa Sh1.2 milioni, Sh740,599 na Sh493,733 mtawalia.