• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 6:50 AM
Mtimkaji wa mbio fupi Makena ashinda kilomita 10 mbio za nyika Nairobi

Mtimkaji wa mbio fupi Makena ashinda kilomita 10 mbio za nyika Nairobi

Na GEOFFREY ANENE

EVANGELINE Makena Kathenya ameibuka mshindi wa mbio za nyika za Nairobi katika kitengo cha kinadada cha kilomita 10 katika uwanja wa Magareza mtaani Nairobi West, Jumamosi.

Stephen Lemayian amezoa taji upande wa wanaume nao Paul Sunte na Caroline Wanjiku wakatawala mbio za chipukizi kilomita nane na sita mtawalia.

Makena, ambaye anafahamika zaidi kwa kukimbia mbio za uwanjani za mita 200 na 400, alikata utepe wa kwanza kwa dakika 35:21.3 akifuatiwa na Lydia Nyasigeta (35:35.9) na Catherine Njihia (35:49.7).

Lemayian alivuna taji baada ya kukamilisha kilomita 10 kwa dakika 29:19.3. Alifuatwa kwa karibu na Aaron Kipkoech (30:02.6) na Brian Kiprop (30:10.3).

Paul Sunte (24:06.3), Franklin Saitoti (24:20.9) na Chris Wanyoike (24:23.2) walifagia nafasi tatu za kwanza katika kitengo cha wanaume wasiozidi umri wa miaka 20 mtawalia.

Nafasi tatu za kwanza za mbio za wanawake wasiozidi umri wa miaka 20 ziliwaendea Wanjiku (19:47.7), Jane Wangare (20:41.3) na Ruth Mwihaki (20:49.5). Nairobi kama tu maeneo mengine 12 na wanachama watano wa Shirikisho la Riadha Kenya (AK), wataingiza wanariadha sita kwenye mashindano ya kitaifa yatakayofanyika Januari 21 katika Chuo cha Mafunzo cha Magereza (PSTC) Ruiru.

  • Tags

You can share this post!

STAA WA SPOTI: Huyu hapa malkia wa uendeshaji baiskeli Kenya

UJAUZITO NA UZAZI: Tatizo la ‘lochia’ baada ya...

T L