• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 5:50 AM
Neymar na Mbappe wabeba PSG dhidi ya Bordeaux ligini

Neymar na Mbappe wabeba PSG dhidi ya Bordeaux ligini

Na MASHIRIKA

NEYMAR alifunga mabao mawili na kusaidia waajiri wake Paris Saint-Germain (PSG) kunyanyasa Bordeaux 3-2 katika Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1).

Fowadi huyo raia wa Brazil aliwaweka PSG uongozini katika kipindi cha kwanza baada ya kushirikiana vilivyo na Kylian Mbappe.

Wawili hao walishirikiana tena kwa ajili ya bao la pili la PSG huku Mbappe alimwandalia Neymar krosi safi kutoka nje ya kijisanduku.

Ingawa Mbappe alifunga bao la tatu, Bordeaux walirejea mchezoni kwa matao ya juu mwishoni mwa kipindi cha kwanza na kufunga mabao mawili ya haraka kupitia Alberth Elis na M’Baye Niang.

Ushindi huo wa PSG chini ya kocha Mauricio Pochettino sasa unawaweka kileleni mwa jedwali la Ligue 1 kwa alama 34 huku pengo la pointi 10 likitamalaki kati yao na nambari mbili Lens.

Nice na Marseille wanafunga orodha ya nne-bora kwa alama 23 na 22 mtawalia.

PSG wanajivunia kampeni za kuridhisha zaidi muhula huu ikizingatiwa kwamba wamepoteza mechi moja pekee kati ya 13 zilizopita ligini huku wakiweza wazi maazimio ya kutwaa taji la Ligue 1 ambalo Lille waliponyoka nalo mnamo 2020-21.

PSG walikosa huduma za nyota Lionel Messi anayeuguza jeraha katika mechi iliyowakutanisha na Bordeaux.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Barcelona walazimishiwa sare ya 3-3 dhidi ya Celta Vigo

Arsenali yafululiza mechi 10 bila kushindwa

T L