NA MASHIRIKA
MANCHESTER, Uingereza
MANCHESTER United na Arsenal watakuwa mawindoni katika mechi kubwa za wikendi hii kulipiza kisasi dhidi ya Manchester City na Tottenham Hotspur kwenye Ligi Kuu ya Ungereza, mtawalia.
‘Mashetani wekundu’ wa United wanaalika mabingwa watetezi City ugani Old Trafford leo alasiri nao wanabunduki wa Arsenal watazuru Tottenham kesho Jumapili.
Masaibu ya Chelsea yaliongezeka Alhamisi usiku walipokung’utwa 2-1 na wenyeji Fulham katika mechi ambayo sajili mpya Joao Felix alianza maisha ugani Stamford Bridge kwa kulishwa kadi nyekundu.
United wamejaa motisha. Wanafukuzia ushindi wa tano mfululizo ligini na saba kwa mpigo katika mashindano yote.Wamepoteza mchuano mmoja katika 18 tangu Erik ten Hag achukue hatamu.
United wana nafasi nzuri ya kung’oa Newcastle kutoka nafasi ya tatu mradi wanyamazishe City ambao wametawala gozi la Manchester mara tatu mfululizo kwa jumla ya mabao 12-4.
Mara ya mwisho United waliponyoka na ushindi dhidi ya City ligini ni 2-0 Machi 2021.
Nambari nne United wanatarajiwa kukaribisha beki Lisandro Martinez katika kikosi cha 11 wa kwanza tangu Kombe la Dunia.
Atashirikiana na mabeki Raphael Varane na Luke Shaw. Beki Aaron Wan-Bissaka anatarajiwa kuhifadhi nafasi yake pembeni kulia kwa sababu kuna hofu kuhusu hali ya Diogo Dalot.
City wanakamata nafasi ya pili, alama tano nyuma ya viongozi Arsenal. Vijana wa kocha Pep Guardiola wamezoa ushindi mara mbili katika michuano minne ya ligi iliyopita.
Watajibwaga uwanjani wakiuguza kipigo cha mabao 2-0 kwenye Kombe la Carabao kutoka kwa Southampton. Guardiola alisema Jumatano kuwa City wataishia kujuta ikicheza ilivyofanya dhidi ya Southampton.
Mhispania huyo anatarajiwa kupigwa jeki na beki John Stones, kiungo Kevin De Bruyne na mshambulizi Erling Haaland katika kikosi kitakachoanza mechi.
Ushindi wa City utawekea presha Arsenal ya kocha Mikel Arteta ambaye pia vijana wake watakuwa na mtihani mgumu dhidi ya nambari tano Tottenham. Siku za kocha Graham Potter katika klabu ya Chelsea huenda zinaelekea kufika ukingoni kufuatia msururu wa matokeo mabovu.
Subscribe our newsletter to stay updated