• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 5:50 AM
Okutoyi achafua Safi na kutinga fainali tenisi ya World Tour Nairobi

Okutoyi achafua Safi na kutinga fainali tenisi ya World Tour Nairobi

Na GEOFFREY ANENE

NYOTA Angella Okutoyi amebandua Meshkatolzahra Safi kwenye mashindano ya tenisi ya World Tour (J4 Nairobi II) baada ya kulemea raia huyo wa Iran kwa seti 2-1 katika nusu-fainali jijini Nairobi, Alhamisi.

Okutoyi, ambaye atasherehekea kugonga umri wa miaka 17 hapo Januari 29, alipoteza seti ya kwanza kwa alama 3-6 kabla ya kukung’uta Safi katika seti mbili za mwisho 6-2, 6-2 na kutinga fainali ya mchezaji mmoja kwa mmoja.

Kilikuwa kisasi kitamu kwa sababu Okutoyi alipoteza kwa seti 2-1 dhidi ya Safi katika nusu-fainali ya mashindano ya daraja ya chini kabisa J5 Nairobi mwaka 2019.

Mkenya huyo, ambaye anashirikiana na Safi katika tenisi ya wachezaji wawili kila upande, atakabiliana na raia wa Hungary Luca Udvardy katika fainali ya Ijumaa.

Mwanatenisi Angella Okutoyi akiwa Nairobi Januari 22, 2021. Picha/ Sila Kiplagat

Fainali hiyo inatarajiwa kuwa moto na mtihani mkubwa wa Okutoyi, hasa kwa sababu italeta pamoja wacheza wawili wanaorodheshwa juu katika mashindano haya. Okutoyi,16, ndiye nambari moja katika mashindano haya katika nafasi ya 151 duniani naye Udvardy, 15, ni wa pili katika nafasi ya 195 duniani.

Okutoyi alipaa nafasi 35 baada ya kushinda duru ya kwanza (J4 Nairobi I) iliyofanyika Januari 18-23 naye Udvardy aliteremka nafasi tatu kwa kufanya vibaya katika duru hiyo. Wawili hawa hawajawahi kukutana katika historia yao.

Okutoyi atashirikiana na Safi katika fainali ya wachezaji wawili wawili dhidi ya Olga Mishenina (Urusi) na Maria Ustic (Uingereza) hapo Ijumaa.

You can share this post!

Madiwani zaidi ya 50 Murang’a waelezea kuunga BBI

Uhuru akalia makaa ya moto