OMBI limetolewa kwa uhusiano mzuri wa soka baina ya klabu za sehemu za mwambao wa Pwani wa Afrika Mashariki urudiwe mara tatizo la corona litakapomalizika kwani uhusiano huo ulisaidia pakubwa maendeleo ya mchezo huo.
Akizungumza na Taifa Leo jana, Mkurugenzi wa Ufundi wa Cosmos FC Aref Baghazally alisema ulipokuwako uhusiano wa kisoka baina ya klabu maarufu za miji ya Pwani ya Afrika Mashariki yakiwemo Mombasa, Dar es Salaam, Tanga na Zanzibar, mchezo huo uliimarika.
“Tulikuwa tukifurahikia kuziona timu kutoka Pwani ya Tanzania zikifika hapa kucheza na timu zetu maarufu za Liverpool (Mwenge) na Feisal na mara nyingine hata sisi tilkuwa tukifika huko Bongo timu zetu zinapokwenda kucheza mechi za kirafiki ama mashindano,” akasema Baghazally.
Timu ambazo zilikuwa na ushirikiano mkubwa kisoka ni za Mombasa za Liverpool (Mwenge) na Feisal na zile za Tanzania ambazo ni Young Africans na Sunderland (sasa Simba) za Dar, African Sports na Coastal Union za Tanga na Vikokotoni ya Zanzibar.
Baghazally ambaye aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa klabu tatu za zamani za Ligi Kuu ya kenya, Coast Stars, Congo United na Dubai Bank FC amesema uhusiano wa klabu baina ya sehemu hizo za Pwani unastahili kuanzishwa upya kwa klabu zilizoko wakati huu.
Alitoa ombi kwa wahisani wajitokeze kuisaidia timu ya Congo Boys FC ipate udhamini wa kutosha na ipiganie nafasi ya kupanda kutoka Ligi ya Taifa Daraja la Kwanza hadi Supaligi ya Taifa.