• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 AM
PSG waambulia sare tasa dhidi ya Reims ligini

PSG waambulia sare tasa dhidi ya Reims ligini

Na MASHIRIKA

BEKI Sergio Ramos alionyeshwa kadi nyekundu kwa mara ya 28 katika taaluma yake ya usogora wakati wa mechi ya Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1) iliyoshuhudia waajiri wake Paris Saint-Germain (PSG) wakiambulia sare tasa dhidi ya Reims mnamo Jumamosi usiku.

Difenda huyo wa zamani wa Real Madrid alionyeshwa kadi mbili za manjano kwa kumgombeza refa dakika chache kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa kipindi cha kwanza kupulizwa.

PSG waliokosa huduma za Lionel Messi anayeuguza jeraha, walimtegemea pakubwa kipa Gianluigi Donnarumma aliyepangua makombora na fataki nzito alizoelekezewa na fowadi matata wa Reims, Arber Zeneli.

Neymar na Kylian Mbappe pia walionyeshwa kadi nyekundu katika pambano hilo. Ni mara ya pili msimu huu ambapo PSG wamepoteza alama katika kampeni za Ligue 1.

Mabingwa hao watetezi wanaselelea kileleni mwa jedwali kwa alama 26, tatu zaidi kuliko nambari mbili Olympique Marseille waliopigwa 2-1 na limbukeni Ajaccio mnamo Jumamosi.

Reims ambao wameshinda mechi moja pekee kati ya 10 zilizopita msimu huu, wanashikilia nafasi ya 14 jedwalini kwa pointi nane sawa na Nice, Auxerre na Angers.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Harry Kane aongoza Spurs kucharaza Brighton katika mchuano...

Ruto ayataka mataifa ya EAC kuondoa vikwazo vya kibiashara...

T L