• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:31 PM
Ronaldo ashindwa kutambisha Ureno dhidi ya Serbia

Ronaldo ashindwa kutambisha Ureno dhidi ya Serbia

Na MASHIRIKA

CRISTIANO Ronaldo alishindwa kutambisha Ureno katika mechi ya Kundi A iliyoshuhudia wenyeji Serbia wakiwalazimishia mabingwa hao wa bara Ulaya sare ya 2-2.

Fowadi Diogo Jota wa Liverpool alifungia Ureno mabao mawili ya kichwa kabla ya Serbia kutoka nyuma na kusawazisha mambo kupitia Aleksandar Mitrovic na Filip Kostic.

Ronaldo alidhani alikuwa amefungia Ureno bao la ushindi mwishoni mwa kipindi cha pili ila refa akashikilia kwamba mpira aliouelekeza langoni mwa Serbia haukuvuka mstari wa goli.

Hatua hiyo ilimfanya fowadi huyo wa Juventus kutupa chini utepe wake wa unahodha na kuondoka uwanjani Rajko Mitic kwa hasira.

Serbia walikamilisha mchuano huo wakiwa na wachezaji 10 pekee ugani baada ya Nikola Milenkovic kuonyeshwa kadi nyekundu kwa hatia ya kumchezea visivyo mwanasoka Danilo Pereira wa FC Porto.

Mechi ilikuwa ya 1,000 kwa kocha wa Ureno, Fernando Santos kusimamia na ilimpa Mitrovic jukwaa la kumpiku Stjepan Bobek na kuwa mfungaji bora wa muda wote nchini Serbia (mabao 39).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Afisa wa afya wa Nakuru azikwa

Ivory Coast na Morocco wajikatia tiketi za kushiriki...