• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:31 PM
Rovanpera mfalme mpya Safari Rally, Toyota iking’aa

Rovanpera mfalme mpya Safari Rally, Toyota iking’aa

Na GEOFFREY ANENE

NYOTA ya dereva chipukizi Kalle Rovanpera iliendelea kung’aa baada ya kuponyoka na taji la duru ya sita ya Mbio za Magari za Dunia (WRC) Safari Rally katika eneobunge la Naivasha, Jumapili.

Ni ushindi wake wa nne katika WRC msimu huu baada ya Uswidi, Croatia na Ureno. Anaongoza msimu kwa alama

Akishirikiana na raia mwenzake kutoka Finland Jonne Halttunen katika gari la Toyota GR Yaris, Kalle alikamilisha kilomita 363.44 za mashindano kwa saa 3:40:24.9 katika eneo la Hell’s Gate.

Rais Uhuru Kenyatta, ambaye alianzisha mbio hizo Juni 23 nje ya Jumba la KICC jijini Nairobi na Mama wa Taifa Margaret Kenyatta waliwatuza. Nafasi hiyo ni hatua kubwa kutoka nambari sita ya mwaka jana.

Amaanraj Rai akishirikiana na Gugu Panesar alikuwa Mkenya wa kwanza katika nafasi ya 13 akifuatiwa na Evans Kavisi/Absalom Aswani na bingwa wa Afrika na Kenya 2021 Carl Tundo/Tim Jessop katika nafasi ya 14 na 15 mtawalia.

Maxine Wahome akielekezwa na Murage Waigwa alishinda kitengo cha WRC3 katika nafasi ya 22 kwa jumla. Bingwa huyo wa Lioness Rally alipongezwa na Rais Kenyatta akaahidi kuwa ataendelea kusaidiwa.

Maxine alifuatiwa katika kitengo hicho na Hamza Anwar/Adnan Din (24 kwa jumla), Jeremiah Wahome/Victor Okundi (25) na McRae Kimathi/Mwangi Kioni (27). Wanne hao wako katika mradi wa chipukizi kukuzwa na Shirikisho la Mbio za Magari Duniani (FIA).

Kimathi anayeshiriki duru zote sita za Mbio za Magari za Dunia za chipukizi (JWRC), sasa ataelekeza juhudi zake nchini Estonia mnamo Julai 14-17.

Kalle, ambaye babake Harri Rovanpera alishiriki Safari Rally mara nne bila kutwaa taji, alifuatwa na wenzake kutoka timu ya Toyota Elfyn Evans kutoka Wales/Martin Scott (3:41.17.7), Mjapani Takamoto Katsuta/Aaron Johnston (3:42:07.6) na bingwa wa 2021 Sebastien Ogier/Benjamin Veillas kutoka Ufaransa (3:42:35.2).

Mbelgji Thierry Neuville/Martijn Wydaeghe alikuwa dereva wa kwanza asiyetoka Toyota akiambulia nafasi ya tano (3:51:05.8). Alipaisha Hyundai i20 N.

Bingwa wa 2021 Ogier alishinda mikondo ya kwanza, tano, sita na 13, Neuville akatawala mikondo ya tisa, 10 na 19 (mwisho) na Rovanpera akaonyesha wenzake kivumbi mikondo ya tatu, nne, saba, 12 na 15.

Wengine waliopata ushindi wa mikondo ni Sebastien Loeb (pili, 17 na 18), Elfyn (nane na 11), Adrien Fourmaux (14) na Ott Tanak (16).

Ogier, Rovanpera na Evans wanapeperusha bendera ya Toyota GR Yaris, Loeb na Fourmaux wako M-Sport Ford nao Neuville na bingwa wa duru ya Italia Tanak ni wa Hyundai i20 N.

Raia wa Poland, Kajetan Kajetanowicz akielekezwa na Maciej Szczepaniak aliibuka mshindi wa WRC2.

  • Tags

You can share this post!

Masaibu ya Sonko sasa yachochea marekebisho kwenye Katiba

Hii ya Ronaldo kuenda Chelsea ni hatari!

T L