• Nairobi
  • Last Updated May 20th, 2024 9:16 PM
Southampton wapiga Arsenal breki kali katika gozi la EPL ugani St Mary’s

Southampton wapiga Arsenal breki kali katika gozi la EPL ugani St Mary’s

Na MASHIRIKA

ARSENAL walipoteza alama muhimu katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa mara ya pili msimu huu baada ya Southampton kuwalazimishia sare ya 1-1 ugani St Mary’s.

Ilikuwa mara ya kwanza baada ya mechi 28 kwa Arsenal kuambulia sare katika EPL tangu wakabwe koo na Burnley waliotoka nao 0-0 ugani Emirates mnamo Januari mwaka huu wa 2022.

Kiungo Stuart Armstrong alisawazishia Southampton katika dakika ya 65 na kufuta juhudi za Granit Xhaka aliyewaweka Arsenal kifua mbele katika dakika ya 11.

Huku Southampton wakiendeleza rekodi nzuri ya kutopigwa katika mechi tatu mfululizo, kasi ya Arsenal ilipigwa breki kali ikizingatiwa kuwa walishuka dimbani wakilenga kudumisha pengo la alama nne kileleni mwa jedwali la EPL.

Masogora hao wa kocha Mikel Arteta walitamalaki mechi katika kipindi cha kwanza ila wakapoteza nafasi nyingi za wazi kupitia kwa Gabriel Martinelli, Bukayo Saka, Martin Odegaard na Gabriel Jesus waliomshughulisha kipa Gavin Bazunu.

Hata hivyo, Southampton waliimarisha mchezo katika kipindi cha pili huku ushirikiano mkubwa kati ya Armstrong na Mohamed Elyounoussi ukitatiza safu ya nyuma ya Arsenal waliowajibisha Kieran Tierney, Eddie Nketiah na Fabio Vieira katika kipindi cha pili.

Sare hiyo ilinufaisha zaidi mabingwa watetezi wa EPL, Manchester City, waliokomoa Brighton 3-1 mnamo Jumamosi ugani Etihad. Pengo la pointi mbili ndilo sasa linatenganisha Man-City na Arsenal wanaoselelea kileleni mwa jedwali.

Southampton wanakamata nafasi ya 15 kwa alama 12 sawa na Aston Villa walioponda Brentford 4-0. Chelsea wanafunga mduara wa nne-bora kwa pointi 21, moja kuliko nambari tano Manchester United waliowalazimishia sare ya 1-1 mnamo Jumamosi ugani Stamford Bridge.

Fulham walicharaza Leeds United 3-2 ugani Elland Road nao Leicester City wakapokeza Wolverhampton Wanderers kichapo cha 4-0 uwanjani Molineux katika mechi nyingine za EPL mnamo Oktoba 23, 2022.

  • Tags

You can share this post!

Wakazi wataka KWS iwasaidie kuondoa majoka yaliyowavamia

Urusi sasa yalenga vituo vya umeme nchini Ukraine

T L