• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 1:14 PM
Spurs wataka Man-City iwape Sh24.9 bilioni kwa ajili ya Harry Kane

Spurs wataka Man-City iwape Sh24.9 bilioni kwa ajili ya Harry Kane

Na MASHIRIKA

KOCHA Nuno Espirito Santo amesema bado hajazungumza na fowadi Harry Kane ambaye amewataka waajiri wake Tottenham Hotspur kumpa idhini ya kuondoka ili atafute hifadhi mpya kwingineko.

Kane ambaye pia ni nahodha wa timu ya taifa ya Uingereza, alikosa mechi ya kirafiki iliyowakutanisha Spurs na Chelsea mnao Agosti 4, 2021. Gozi hilo la kupimana nguvu lilikamilika kwa sare ya 2-2 ugani Stamford Bridge.

Kane, 28, anahusishwa pakubwa na uwezekano wa kutua Manchester City ambao wako radhi kuweka mezani kima cha Sh15.6 bilioni badala ya Sh24.9 bilioni zinazodaiwa na Spurs.

“Natarajia kuwa na kikao kirefu na Kane. Bado sijapata nafasi hiyo. Inalazimu nijadiliane naye kwa kina kuhusu mustakabali wake,” akasema Nuno aliyepokezwa mikoba ya Spurs mnamo Julai 2021.

Hadi kufikia sasa, Kane amefungia Spurs jumla ya mabao 221.

Kwa mujibu wa gazeti la The Sun, Kane angali likizoni baada ya kuyoyomea Florida, Amerika pamoja na familia yake mwishoni mwa kampeni za Euro 2020.

Wakicheza dhidi ya Chelsea kirafiki, Spurs walifungiwa mabao na Lucas Moura pamoja na Steven Bergwijn baada ya Hakim Ziyech kufungia waajiri wake magoli mawili.

Mechi hiyo iliwapa Spurs fursa ya kumwajibisha kipa Pierluigi Gollini kwa mara ya kwanza tangu akamilishe uhamisho wake hadi Atalanta kwa mkopo mnamo Julai 2021.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Tujiandae kwa Olimpiki za Paris 2024 sasa – Namcos

Messi kuondoka Barcelona