Na JOHN KIMWERE
VIHIGA Queens ingali kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Soka ya Wanawake licha ya kutoka sare tasa na Gaspo Women ugani Mumias Complex.
Nao mabingwa watetezi, Thika Queens ilijikuta kwenye wakati mgumu ilipozabwa bao 1-0 na Ulinzi Starlets ugani Ruaraka, Nairobi.
Mechi hiyo ilianza vyema huku Ulinzi Starlets ya kocha, Joseph Wambua ilionyesha soka safi ndani ya kipindi cha kwanza.
Ulinzi chini ya nahodha Diana Shakava, ilipoteza nafasi mbili safi kupitia Emily Auma aliyechanja mkwanju wa penalti dakika ya 18.
Dakika saba baadaye naye Landline Aoko alipoteza nafasi ya wazi alipobakia na kipa lakini wapi alishindwa kujuma ngozi ya ng’ombe ndani ya wavu.
Sawa na wapinzani wao Thika Queens chini ya kocha, Bertha Achieng itajilaumu baada ya Stella Adhiambo kupoteza nafasi mbili za wazi.
Ulinzi ilipata bao la ushindi kupitia juhudi zake Lucy Akoth kunako dakika ya 78.
”Ninashukuru Mungu kwa baraka zake. Amenibariki na mtoto kijana pia wachezaji wangu wamenipa ushindi mtamu wa alama tatu muhimu kwenye mechi zetu,” kocha wa Ulinzi alisema na kutoa wito kwa vipusa wake kuendeleza mtindo kwenye juhudi za kuwania taji hilo.
Kwenye matokeo mengine ya mechi hizo, Kangemi Starlets kwa mara nyingine iliteleza na kushindwa kusajili ushindi wa kwanza ilipozabwa mabao 4-3 na Zetech Sparks, Wadadia iliandikisha ushindi wa mabao 2-0 mbele ya Kayole Starlets huku Bunyore Starlets ikidungwa bao 1-0 na Kisumu Allstarlets.
Nazo Trans Nzoia Falcons na Nakuru City Queens ziliumiza nyasi bure baada ya kutoka nguvu sawa kwa sare tasa.
MATOKEO YOTE
Ulinzi Starlets 1-0 Thika Queens
Vihiga Queens 0-0 Gaspo Women
Kisumu Allstarlets 1-0 Bunyore Starlets
Kangemi Starles 3-4 Zetech Sparks
Transnzoia Falcons 0-0 Nakuru City Queens
Wadadia 2-0 Kayole Starlets