Na MASHIRIKA
ARSENAL watamenyana na Wolfsburg katika robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).
Vipusa wa Arsenal watakuwa wenyeji wa mkondo wa kwanza mnamo Machi 22 au 23 huku marudiano yakiandaliwa Machi 30 au 31, 2022. Mshindi wa mechi hizo za mikondo miwili ataingia nusu-fainali dhidi ya Real Madrid au mabingwa watetezi Barcelona watakaovaana kwenye robo-fainali nyingine itakayokutanisha vikosi viwili vya Uhispania.
Bayern Munich watachuana na Paris St-Germain (PSG) huku Juventus wakimenyana na Lyon. Arsenal walitinga hatua ya muondoano kwa wingi wa mabao licha ya kupepetwa 4-1 na Hoffenheim katika mchuano wa mwisho wa hatua ya makundi. Kichapo cha 5-0 kutoka kwa Hoffenheim kingedengua The Gunners.
Wolfsburg walibandua wanafainali wa msimu wa 2020-21, Chelsea kwa kichapo cha 4-0 katika mchuano wa mwisho wa makundi. Arsenal ndicho kikosi cha pekee kutoka Uingereza kuwahi kutwaa taji la UEFA baada ya kufanya hivyo mnamo 2007. Wolfsburg walitia kapuni taji hilo mnamo 2013 na 2014 mtawalia.
Miamba hao wa Ujerumani walidengua Arsenal kwenye nusu-fainali mnamo 2012-13 na kuishia kutwaa ubingwa. Juventus watakuwa wakinogesha robo-fainali za UEFA kwa mara ya kwanza. Mshindi atafuzu kumenyana na Bayern ambao ni malkia wa Ujerumani au mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Ufaransa, PSG.
Droo ya robo-fainali za UEFA:
Bayern Munich vs Paris St-Germain
Juventus vs Lyon
Arsenal vs Wolfsburg
Real Madrid vs Barcelona