• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 10:50 AM
Wawira ashindia Kenya medali ya shaba Birmingham unyanyuaji uzani walemevu

Wawira ashindia Kenya medali ya shaba Birmingham unyanyuaji uzani walemevu

Na GEOFFREY ANENE

MNYANYUAJI uzani mlemavu Hellen Wawira ameshindia Kenya medali ya shaba mnamo Alhamisi jioni kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola inayoendelea mjini Birmingham, Uingereza.

Mkazi huyo wa kaunti ya Embu, ambaye alianza fani hii baada ya kukamilisha masomo ya shule ya upili mwaka 2014, amenyakua medali hiyo baada ya kuzoa pointi 98.5 kutokana na kuinua kilo 95 na 97 katika majaribio yake mawili ya kwanza.

Wawira, ambaye alishiriki michezo ya Jumuiya ya Madola mjini Gold Coast nchini Australia mwaka 2018 bila kupata medali, alimaliza nyuma ya Waingereza Zoe Newson na Olivia Broome waliovuna pointi 102 na 100 mtawalia katika kitengo hicho cha wanyanyuaji wasiozidi uzani wa kilo 41 (Lightweight).

Wawira, 29, ambaye shujaa wake ni mnyanyuaji mlemavu Mkenya Gabriel Magu, amewahi kushiriki Kombe la Dunia mara mbili na alikuwa katika Olimpiki jijini Tokyo, Japan, mwaka 2021.

Kenya inawakilishwa na jumla ya wachezaji 127 katika fani 16 zikiwemo uogeleaji, raga ya wachezaji saba kila upande wanaume, voliboli ya ufukweni na riadha.

You can share this post!

Biden hajapona corona, daktari wake asema

NDIVYO SIVYO: Kutofaa kwa matumizi ya ‘iko’ kwa maana...

T L