• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
BBI: Reggae yazimwa kwa mara ya tatu

BBI: Reggae yazimwa kwa mara ya tatu

NA BENSON MATHEKA

Kwa mara ya tatu juhudi za kubadilisha Katiba ya Kenya ya 2010 zimegongwa mwamba Mahakama Kuu ilipozima mchakato wa BBI ulioanzishwa na Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga.

Hii ilikuwa mara ya pili kwa juhudi anazoshiriki Bw Odinga kubadilisha katiba aliyopigania kukosa kufua dafu. Mnamo 2015 akishirikiana na vinara wenzake katika uliokuwa muungano wa Cord, walianzisha mchakato wa Okoa Kenya kwa lengo la kubadilisha Katiba.

Walikusanya saini kutoka kwa wafuasi wao walizowasilisha kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC). Hata hivyo, tume ilizima mchakato huo ikisema haukuungwa mkono na wapigakura 1 milioni inavyohitajika kikatiba.

Mnamo 2019, chama cha Third Way Alliance kikiongozwa na wakili Ekuro Aukot, kiliwasilisha mswada wa kubadilisha katiba wa Punguza Mzigo uliolenga kupunguza idadi ya wabunge miongoni mwa mapendekezo mengine ya kupunguza gharama ya kuendesha serikali na kukabili ufisadi ili kutenga pesa zaidi za maendeleo.

Mswada huo ulipata umaarufu na kupiga hatua baada ya IEBC kuamua uliungwa na zaidi ya wapigakura 1 milioni. Hata hivyo, vigogo wa kisiasa nchini akiwemo Bw Odinga waliupinga na kushawishi madiwani katika kaunti zilizo ngome zao kuukataa.

Lengo la Bw Odinga na wenzake kukataa mswada huo ni kuwa ulipunguza nyadhifa serikalini ambazo wanasiasa hutumia kujinufaisha.

Mswada wa Punguza Mzigo, ulishika kasi wakati kamati ya BBI iliyoundwa na Rais Kenyatta na Bw Odinga ilikuwa ikiendelea kukusanya maoni kutoka kwa umma.

Bw Odinga aliwataka wanasiasa wa chama chake kuunga BBI badala ya Punguza Mzigo kwa kuwa ilibuni nyadhifa zaidi za uongozi yakiwemo maeneobunge zaidi.

Hata hivyo, licha ya mswada wa BBI kupiga hatua hadi ukafika bungeni, juhudi za kubadilisha katiba ya 2010 zilitibuka kwa mara ya tatu. Kulingana na wataalamu wa katiba, kutibuka kwa juhudi kubadilisha katiba mara tatu kunaonyesha kwamba walioandika katiba ya 2010 walihakikisha haingevurugwa kwa urahisi na viongozi ili kutimiza maslahi yao ya kibinafsi dhidi ya raia wa kawaida.

“ Msingi uliowekwa katika katiba ya 2010 unaikinga ili isibadilishwe kiholela kutimiza maslahi ya wachache walio mamlakani. Hii ilijitokeza wazi katika uamuzi wa majaji watano Alhamisi,” asema wakili na mwanaharakati Waikwa Wanyoike.

Wakili Ahmednassir Abdullahi alisema kwamba uamuzi ni onyo kwa Rais Kenyatta kwamba Wakenya sio watumwa wake. “ Kwa muhtsari uamuzi wa majaji watano unamaanisha: “Bw Rais, wewe sio Mfalme na Wakenya sio watumwa wako. Mamlaka Makuu ni ya Wanjiku,” alisema Bw Ahmednassir kupitia Twitter

You can share this post!

Mwanamitindo chipukizi kuwakilisha Kenya katika mashindano...

Mogotio United yazidi kung’aa