• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 5:07 PM
CHARLES WASONGA: IEBC iruhusu Wakenya wote walio ughaibuni wapige kura

CHARLES WASONGA: IEBC iruhusu Wakenya wote walio ughaibuni wapige kura

Na CHARLES WASONGA

KULINGANA na takwimu zilizotolewa na Benki Kuu ya Kenya (CBK) mwezi jana, Wakenya wanaoishi na kufanya kazi katika mataifa ya ng’ambo walituma nyumbani Sh341 bilioni mnamo 2020.

Kiwango hiki kinawakilisha ongezeko la asilimia 10.7 zaidi ya Sh308 bilioni walizotuma nchini mnamo 2019.Wakenya wanaoishi nje waliongeza kiwango cha pesa wanazotuma nyumbani licha ya makali ya ugonjwa hatari wa Covid-19 yaliyovuruga chumi za mataifa yote ulimwenguni.

Pesa hizi huwekezwa katika miradi na mipango mbalimbali ya maendeleo humu nchini kando na kugharamia mahitaji mbali mbali ya Wakenya hawa.

Kwa hivyo, Wakenya hawa wana usemi kuhusu namna pesa wanazotuma nyumbani hutumika na serikali iliyoko mamlakani ambayo hukusanya ushuru kutoka kwa miradi na mipango wanayofadhili.

Chini ya kivuli hiki, wenzetu hawa, wapatao 3.5 milioni, wanaoishi na kufanya kazi katika mataifa mbalimbali wana haki ya kushiriki, hususan, katika uchaguzi wa urais.

Isitoshe, baadhi yao hufadhili vyama vya kisiasa na baadhi ya wagombeaji viti mbalimbali.Kwa hivyo, sikubaliani na tangazo la Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwamba ni Wakenya wanaoishi katika mataifa 11 pekee ndio wataruhusiwa kushiriki uchaguzi wa urais 2022.

Mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati alisema kuwa wenzetu wanaoishi Amerika ni miongoni mwa wale ambao wataruhusiwa kujisali kuwa wapiga kura kwa ajili ya kupiga kura za urais.

Wengine watakaoruhusiwa kushiriki shughuli hii ya kidemokrasia ni wale wanaoishi Canada, Uingereza, Muungano wa Milki za Kiarabu (UAE), Qatar na Sudan Kusini.Katika chaguzi za 2013 na 2017 ni Wakenya 3,000 pekee walioko Tanzania, Uganda, Rwanda, Afrika Kusini waliruhusiwa kupiga kura ya urais.

IEBC inafaa kuweka mikakati ya kuhakikisha kuwa itakapoanza shughuli ya usajili wa wapiga kura wapya mnamo Oktoba 4, 2021 Wakenya katika mataifa yote ambako Kenya ina afisi za ubalozi waruhusiwe kushiriki.

Shughuli hiyo ya usajili iendeshwe katika afisi hizo za kibalozi chini ya usimamizi wa maafisa wa serikali wanaohudumu katika mataifa husika.

IEBC inalenga kusajili jumla ya wapiga kura wapya 9.2 milioni, miongoni mwao ikiwa ni vijana 5.2 milioni ambao watakuwa wametimu umri wa miaka 18 kufikia 2022.

Kwa hivyo, itakuwa makosa kwa IEBC kupuuza sehemu kubwa ya Wakenya 3.5 milioni walioko katika mataifa ya nje kando na 11 ambayo Bw Chebukati alitaja wiki jana.

Hii ni licha ya kwamba watu hawa hutuma mabilioni ya fedha nchini kupiga jeki shughuli za maendeleo.Kuishi au kufanya kazi mataifa ya nje kusiwe sababu ya kumnyima Mkenya haki yake ya Kikatiba ya kushiriki shughuli za kidemokrasia nchini.

IEBC iruhusu Wakenya wote wanaoishi ughaibuni wajisajili kuwa wapiga kura ili washiriki uchaguzi mkuu ujao.

You can share this post!

Wataalamu wanaonya dhidi ya kutumia tembe za P2 kiholela

CECIL ODONGO: Yashangaza mno wazee kutawaza watu kiholela