• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 6:50 AM
Hatimaye Shahbal akubali kuunga Nassir ugavana

Hatimaye Shahbal akubali kuunga Nassir ugavana

CECIL ODONGO NA IBRAHIM ORUKO

CHAMA cha ODM jana kilionekana kuimarisha mikakati ya kuifungia UDA katika siasa za Mombasa baada ya mfanyabiashara Suleiman Shahbal kukubali kumuunga mkono mbunge wa Mvita Abdulswamad Sheriff Nassir kuwania kiti cha Ugavana mnamo Agosti 9 mwaka huu.

Kinara wa ODM Raila Odinga jana alishiriki katika kikao na wanasiasa hao wawili pamoja na wenzao kutoka Mombasa katika Jumba la Orange, ambapo Bw Shahbal alikubali kutupilia mbali azma yake. Mfanyabiashara huyo sasa atajiunga na kampeni za kitaifa za Urais wa waziri huyo mkuu wa zamani.

Akihutubu wakati wa kikao hicho, Bw Odinga alisema kuwa Seneta wa sasa Mohammed Faki atatetea kiti chake kupitia ODM na kuonyesha matumaini yake kuwa ODM bado itadumisha ubabe wake katika siasa za Mombasa.

“Namshukuru Shahbal kwa kukubali kumuachia Abdulswamad Nassir nafasi ya kuwania kiti cha ugavana kwa tiketi ya ODM. Pia Bw Faki atatetea kiti chake kupitia ODM kwenye uchaguzi mkuu ujao.

“Nawashukuru wafuasi wetu Mombasa kwa kuwa na subira na kuwa nyuma ya chama wakati ambapo majadiliano kuhusu suala hili yalipokuwa yakiendelea,” akasema Bw Odinga.

“Sasa ODM ipo tayari kumenyana na vyama vingine Agosti 9. Nawashuru sana wafuasi wetu,” akaongeza Bw Odinga.

Bw Shahbal alikuwa amewania kiti cha ugavana wa Mombasa mnamo 2013 kwa tiketi ya Wiper na kisha 2017 kupitia Jubilee, lakini akabwagwa na Bw Joho katika chaguzi hizo zote.

Mnamo Juni mwaka jana, alihama Jubilee na kurejea ODM ili kujiweka pazuri kurithi nafasi ya ugavana baada ya muhula wa pili wa Bw Joho kutamatika Agosti 9 mwaka huu.

Kwa muda wote tangu kurejea kwake ODM, amekuwa akisisitiza kuwa chama hicho lazima kiandae uteuzi huru, kauli ambayo alikariri wiki jana wakati wa mchujo wa nyadhifa za udiwani katika Kaunti ya Mombasa.

Inaaminika Bw Shahbal alishawishiwa kuzima azma yake baada ya matokeo ya kampuni mbalimbali za utafiti kumweka Bw Nassir mbele yake.

Ingawa aliyapinga matokeo hayo, inasemekana Bw Odinga jana alimshawishi azime azma yake na kumshirikisha katika kampeni zake za kitaifa.

Viongozi waliohutubu katika kikao cha jana – akiwemo Mabw Joho, Faki na Mwenyekiti wa ODM Kaunti ya Mombasa, Mohammed Khamis – walimrejelea Bw Shahbal kama kiongozi aliye na sifa za kuwa gavana lakini akaweka chama mbele.

 

  • Tags

You can share this post!

Kocha wa Bayern asema anatishiwa maisha baada ya kikosi...

Suluhu kuzindua filamu yake Amerika kuvutia watalii kuzuru...

T L