Na Wanderi Kamau
LICHA ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga, kupigia debe Mpango wa Maridhiano (BBI), kuna viongozi na wanaharakati waliojitokeza wazi kuupinga mchakato huo.
Miongoni mwao ni kiongozi wa chama cha Narc-Kenya, Bi Martha Karua, mwanaharakati David Ndii, John Githongo, Gavana Kivutha Kibwana (Makueni), chama cha Thirdway Alliance, mrengo wa Tangatanga (ambao humuunga mkono Naibu Rais Dkt William Ruto) kati ya wengine.
Bi Karua aliwakosoa vikali Rais Kenyatta na Bw Odinga, akisema wanapaswa kutekeleza Katiba ya sasa badala ya kuanza mchakato wa kuifanyia marekebisho ili “kujifaidi wao wenyewe”.
“Ni makosa kwa wawili hao kuiteka Katiba ya nchi na kuifanya kama mali yao. Rais anapaswa kutekeleza Katiba ya 2010. Hatuhitaji mageuzi yoyote ya kisheria kwani Kenya haina mgogoro wowote wa kikatiba. Changamoto kuu tulizo nazo ni mtindo wa serikali kukwepa utekelezaji wa maagizo ya mahakama,” akasema Bi Karua.
Mwanasiasa huyo aliungana na wanaharakati wengine kutoka Kituo cha Sheria kuwasilisha kesi kortini kupinga mchakato huo.
Mrengo wa ‘Tangatanga’ ulitoa kauli kama hizo, ukisema kuna masuala mengi muhimu yanayopaswa kushughulikiwa nchini badala ya mpango huo.Miongoni mwa viongozi wa mrengo huo waliopiga kura ya ‘La’ kuipinga ripoti ni wabunge Ndindi Nyoro (Kiharu), Kimani Ichung’wa (Kikuyu), Rigathi Gachagua (Mathira) kati ya wengine.