Na GEORGE ODIWOUR
ALIYEKUWA gavana wa Nairobi, Dkt Evans Kidero, ameshutumu baadhi ya wanasiasa katika Kaunti ya Homa Bay kwa kutumia magenge ya wahuni kuhangaisha wapinzani wao.
Dkt Kidero alisema wahuni hao hufika katika mazishi na mikutano ya kisiasa kuzomea wapinzani wa mfadhili wao.
Kulingana na gavana huyo wa zamani, wahuni hao huvuruga hotuba kwa kupuliza vifaa vya vuvuzela.
“Lengo lao ni kuhakikisha kuwa watu waliokusanyika wanakosa kusikiliza mambo yanayosemwa na mwanasiasa anayedhaniwa kuwa tishio kwa mfadhili wao,” alieleza.
Kaunti ya Homa Bay imekuwa ikikumbwa na visa vya vurugu kila mara uchaguzi unapokaribia.