Na GEORGE MUNENE
SPIKA wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi amewarai vijana wasake vyeo vya uongozi katika uchaguzi mkuu wa 2022.
Bw Muturi ambaye ametangaza kwamba atawania kiti cha Urais katika uchaguzi huo, amewataka vijana wasiogope kuwania vyeo vya uongozi kwa kuwa wao pia wana uwezo wa kuongoza.
Akizungumza katika Kaunti ya Embu Jumamosi jioni, Bw Muturi alisema kuwa idadi ya vijana ni kubwa nchini na wanafaa watumie hilo kuchaguana kwenye vyeo mbalimbali vya uongozi katika viwango vya kaunti na kitaifa.
Bw Muturi pia aliwashajiisha vijana wajitokeze na kushindana hata na baadhi ya wanasiasa wakongwe ambao wametawala siasa za nchi kwa miaka mingi badala ya kulalamikia ufisadi na kuporomoka kiuchumi ilhali mara nyingi wanahepa kujitosa ulingoni.
“Wakati wa vijana kuongoza ni sasa. Waamke na wawanie vyeo vya kisiasa kwa sababu nina imani watashinda na kupigania mabadiliko wanayoyataka,” akasema.