• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 5:50 AM
Njama ya Tangatanga kutwaa uongozi wa Jubilee

Njama ya Tangatanga kutwaa uongozi wa Jubilee

Na MWANGI MUIRURI

NJAMA kali imepangwa na mrengo wa Naibu wa Rais Dkt William Ruto ya kuchukua udhibiti wa chama cha Jubilee kuanzia Mei 2020 baada ya huduma za maafisa wanaoshikilia nyadhifa za uongozi kutamatika. 

Hii ni baada ya taswira kuendelea kujiweka wazi kuwa huenda Rais Kenyatta akose kutimiza ahadi yake ya tangu 2013 hadi Machi 2018 kuwa angetawala kwa miaka 10 kisha amkabidhi Dkt Ruto usukani kwa miaka mingine 10.

Mrengo huo wa Dkt Ruto unaofahamika kama Tangatanga unanuia kufanyia mabadiliko mpangilio wa chama cha Jubilee katika nyanja za maamuzi ili kuwazima walio na imani kwingine kando na mkondo wea urithi wa Ruto.

“Rais anang’atuka mamlakani 2022 na sheria tulizo nazo kwa sasa hazimpi nafasi ya kuwania wadhifa mwingine wowote.

“Amekuwa akikiri hadharani kuwa hana haja ya kusalia mamlakani kama anavyoshinikizwa na baadhi ya wanasiasa na kawaida ya hali hiyo ni aende nyumbani akapumzike nasi tulio na ajenda za kisiasa za baada ya 2022 tukiwekeza kwa urithi wa Dkt Ruto tubakie usukani,” asema aliyekuwa mwenyekiti wa wawaniaji wa Jubilee Mlima Kenya, Samuel Maina.

Maina anakiri kuwa “huu ni msimu wa siasa, Wakenya hawachoki na siasa na wanazipenda huku nasi tukiwa ni wanasiasa ambao huwezi ukatuzima kuendeleza mikakati yetu ya kujipanga.”

Gavana wa Kiambu, Ferdinand Waititu aliambia Taifa Leo Dijitali kuwa “ndio, tuko na mipango ya kujiimarisha kama chama na kuweka wazi ajenda yetu ya kumuunga mkono Ruto. Ndio sababu kumechipuka kila aina ya hila na njama katika ulingo wetu wa kisiasa kukizuka mipangilio mipya ya siasa za 2022.”

Alikiri kuwa “Rais tutampa kazi tu ya kutushauri kama aliye na tajiriba ya uongozi nasi tuchukue usukani wa mieleka nyanjani kuhusu urithi wa 2022.”

Hayo yanajiri huku katika siku za hivi karibuni mrengo huo wa Tangatanga ukionekana sasa kumkabili Rais Kenyatta kuhusu kauli zake za kuukemea hadharani kuhusu siasa za mapema za uwaniaji wa 2022.

Tayari, mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro, mwenzake wa Bahati Kimani Ngunjiri na Kimani Ichung’wa wa Kikuyu wamesema kuwa rais hana mamlaka ya kuzima Wakenya kujadiliana kuhusu kesho yao ya kisiasa.

Pia, akiwa katika eneo la Eldama Ravine, Dkt Ruto alisema kuwa “hakuna ubaya wowote kwa sisi kujipanga kuhusu uchaguzi mkuu wa 2022. Hata Wakristo kwa sasa wanajiandaa kwa safari ya Mbinguni hata ikiwa hatujui siku wala saa ya kutimia kwa safari hiyo.”

Aidha, amesema kuwa chama cha Jubilee kitaandaa mkutano wa pamoja wa kujipanga “na kuwaondoa abiria walio tu na mazoea ya kutupigia kelele na kuendeleza masuala ya chama katika mikutano ya matanga na vbyombo vya habari.”

Kauli hiyo ya Ruto inaonekana waziwazi kuwa jibu kwa Rais Kenyatta ambaye amekuwa akisisitiza kuwa wanasiasa wanafaa kukoma siasa za 2022 na badala yake wawajibikie kufanikisha maendeleo kwa Wakenya.

Kulingana na wadokezi wetu ndani ya mrengo huo wa Dkt Ruto, njama hiyo ya kuwang’atua wandani wa Kieleweke kutoka ushawishi wa chama itafanikishwa Mei mwaka ujao ambapo kandarasi ya uongozi ya maafisa wa chama hicho itatamatika na kuhitajika kuandaliwa kwa uchaguzi wa chama.

Katika mpangilio wa kisasa, Rais Kenyatta na Dkt Ruto wameorodheshwa kama kiongozi na naibu wa chama cha Jubilee mtawalia.

Katibu Mkuu ni Raphael Tuju ambaye pia analengwa kung’atuliwa na pia nafasi ya Naibu mwenyekiti, David Murathe ijazwe baada yake kujiuzulu mwaka jana baada ya kushinikizwa na Tangatanga ang’atuke alipotangaza hadharani kuwa Jubilee haimuungi mkono Dkt Ruto kwa siasa za 2022.

Nyoro anasisistiza kuwa “ni lazima tupange chama chetu ili kiwe na nafasi bora ya kuwania 2022. Katika kufanya hivyo, wale wote ambao wametuonyesha wazi kuwa hawana Imani na kauli ya wengi kuwa Dkt Ruto ndiye mwaniaji wetu 2022 lazima watapunguziwa usemi wao.”

Bw Nyoro alisema kuwa “kunao wametangaza kuwa chaguo lao la mrithi wa Ikulu 2022 litatushtua hii ikikwa na maana kuwa chaguo hilo sio lile tunalolijua kwa sasa ilihali wengi ndani ya Jubilee tuliamua 2013 kuwa mwaniaji wetu atakuwa ni Dkt Ruto.”

Bw Albert Nyaundi akiwa ni mwanakamati katika bodi ya ushauri wa chama alithibitishia Taifa Leo kuwa kipengele cha awamu ya uongozi ndani ya chama hicho kinatoa mwanya wa uchaguzi wa maafisa wapya mwaka ujao.

Bodi hiyo ya ushauri huwa na maafisa wanaowakilisha vyama 12 vilivyoungana 2017 kuunda chama cha Jubilee.

Mbunge wa Kapseret Oscar Sudi aliambia Taifa Leo Dijitali kuwa “tunangojea siku ya uchaguzi wa chama kwa hamu kuu ndio tujiweke kama chama kilicho na serikali kwa sasa na kinacholenga kuendeleza malengo ya chama ya kusalia mamlakani.”

Alisema kuwa kwa sasa kuna orodha ya watakaowekwa katika nyadhifa za chama wakijumuishwa katika makundi manane yanayozingatia Mikoa ya kabla ya Katiba Mpya kuunda majimbo 47.

“Tunalenga kuwa na majenerali wa chama katika ngome zetu za Mlima Kenya na Rift Valley kisha tuthibiti Nairobi, Pwani na Kaskazini Mashariki kabla ya kujiweka pema katika eneo la Magharibi. Lengo letu ni kuwindana na kinara wa ODM Raila Odinga ambaye ndiye mpinzani wetu mkuu huku tukiondoa sauti za uasi ndani ya chama chetu cha jubilee,” akasema

You can share this post!

Mwanamke ajifungua ndani ya teksi nje ya Nation Centre

Tuelezwe Sh636m za bima kwa afya ya wakongwe zilivyotumika...

adminleo