DERRICK LUVEGA Na CHARLES WASONGA
KWA mara ya kwanza, tangu aondoke mamlakani, Rais mstaafu Uhuru Kenyatta leo Jumamosi amechapa siasa akisisitiza angali anamuunga mkono kiongozi wa Azimio, Raila Odinga.
Akiongea mjini Luanda katika Kaunti ya Vihiga baada ya kuhudhuria mazishi ya aliyekuwa Waziri wa Elimu George Magoha, Bw Kenyatta amesema ni haki yake ya kikatiba kuunga mkono yule anayemtaka.
“Raila ndiye anatuongoza kisiasa wakati huu. Nilimuunga mkono na bado ninamuunga mkono. Analitakia mema taifa hili,” akawaambia wananchi katika mji huo wenye shughuli nyingi.
Lakini Bw Kenyatta amekariri kuwa amestaafu na kwamba hatamani kiti chochote cha kisiasa, akisema Bw Odinga yuko huru kuendelea kusaka wadhifa anaoutaka.